Kardinali Mauro Piacenza, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri, katika
Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo
tarehe Mosi, Januari amewaandikia barua ya wazi mama wazazi wa Mapadre na Majandokasisi,
akiwaomba kutafakari kwa kina dhamana ya Bikira Maria aliyepewa upendeleo wa pekee
hata akakubali kumzaa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu na Kuhani mkuu.
Bikira Maria
kwa njia ya utii na unyenyekevu wake, aliweza kushiriki katika Mpango wa Kazi ya Ukombozi,
kiasi kwamba, akawa ni Mama wa Mungu, Mlango wa mbingu na sababu ya furaha ya waamini.
Kwa upande wake, Kanisa linawaangalia kwa upendo na shukrani kubwa, akina Mama wote
wa Mapadre na Waseminari, wanaoendelea kushiriki kikamilifu katika majiundo ya watoto
wao: kiroho na kimwili, ili waweze kjujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo
na Kanisa lake; wakitambua kwamba, watoto wao kwa njia ya Sakramenti ya araja takatifu
wamekuwa ni marafiki wa Kristo, wanaomwezesha kuendelea kuwepo kati ya wafuasi wake
kwa njia ya Maadhimisho ya Sakramenti mbali mbali za Kanisa.
Kardinali Piacenza
anasema kwamba, hili ni Fumbo kubwa kwa Padre kuwa ni Kristo mwingine, licha ya mapungufu
na kasoro za kibinadamu zinazoendelea kumwandama katika maisha na utume wake. Anakuwa
ni daraja linalowaunganisha waamini pamoja na Kristo aliyezaliwa, akateswa, akafa
na kufufuka siku ya tatu kama yanenavyo Maandiko Matakatifu. Mapadre ni viongozi wa
waamini katika Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa na wanapofundisha Imani na Kweli
za Kikristo. Matendo yote haya ni mwendelezo wa kazi ya Ukombozi iliyoanzishwa na
Yesu Kristo mwenyewe.
Kardinali Piacenza anabainisha kwamba, Familia ni kitovu
cha Sala na upendo; ni shule ya kwanza ya Imani na kitalu cha miito mitakatifu ndani
ya Kanisa; hasa pale Familia za Kikristo zinapokuwa imara katika tunu msingi za maisha
ya kiutu, kimaadili na kiroho. Huu unakuwa ni udongo mzuri unaoweza kukoleza utakatifu
wa maisha miongoni mwa Mapadre na waamini katika ujumla wao. Wazazi, walezi na ndugu
na Jamaa washiriki kikamilifu katika majiundo ya watoto wao ambao ni Mapadre au bado
wako katika majiundo ya kikasisi.
Wawahimize watoto wao kutekeleza wajibu
na dhamana yao ya Kipadre, wakiwaachia uhuru wa kuweza kulijenga Kanisa na kamwe wasiwe
ni vikwazo vya watoto wao Mapadre. Wawasindikize kwa sala na sadaka yao ya kimama;
ili waweze kutekeleza mapenzi ya Mungu kwa ukamilifu zaidi na kwa ajili ya mafao ya
Familia ya Mungu. Wawasaidie watoto wao katika mapambano ya Kiimani, wakijiunganisha
na Sadaka ya Yesu Kristo pale Msalabani.
Kardinali Mauro Piacenza anawakumbusha
akina Mama wa Mapadre na Waseminari kwamba, ulimwengu wa leo ni tambara bovu linalojionesha
kwa namna ya pekee katika kumong'onyoka kwa maadili na utu wema; watu kuendelea kuelemewa
na mawazo mepesi mepesi pamoja na tabia ya ukanimungu. Ni changamoto ambazo pia ziko
mbele ya Mapadre na Waseminari katika majiundo yao ya Kikasisi.
Mama wa Mapadre
wasikate tamaa kuwasindikiza watoto wao katika sala na majitoleo; wawaombee ili waweze
kudumu katika uaminifu, daima wakichuchumilia utakatifu wa maisha. Kanisa linawaombea
Mama wote wa Mapadre ambao wamekwisha kutangulia mbele ya haki wakiwa na tumaini la
ufufuko na maisha ya uzima wa milele kwa kazi njema waliyoifanya kwa ajili ya Kanisa.
Bikira Maria Mama wa Mungu awe Mwombezi wao wa daima katika hija ya maisha yao kiroho
na kimwili.