Wimbo wa shukrani kwa Mwenyezi Mungu, Te Deum, kwa wema na ukarimu wake kwa Mwaka
2012
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alijumuika na waamini waliomiminika kwenye
Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, mwishoni mwa Mwaka 2012 ili kumwimbia
Mungu utenzi wa sifa na shukrani, Te Deum, wakati wa masifu ya jioni, Siku kuu ya
Bikira Maria Mama wa Mungu.
Te Deum ni utenzi wa sifa, shukrani na matumaini
kwa Mungu ambaye amewakirimia waja wake neema na baraka katika hija ya maisha yao
hapa duniani, licha ya magumu, lakini wema wa Mungu unaojionesha kwa njia ya Yesu
Kristo aliyezaliwa, akateswa, akafa na kufufuka utashinda siku moja.
Baba Mtakatifu
anakiri kwamba, si rahisi kuweza kuupokea ukweli huu kutokana na maovu na ukosefu
wa haki msingi za binadamu ni mambo ambayo yanapewa kipaumbele cha pekee, kinyume
kabisa cha huduma ya upendo, uaminifu na uvumilivu; mambo yanayofunikwa, kiasi hata
cha kutoonekana. Mwamini anapaswa kutumia muda wake kwa kufanya tafakari ya kina,
kuabudu ili kufahamu maana na undani wa maisha yake hapa duniani; ni mwaliko wa kutubu
na kuongoka.
Waamini wanaalikwa kuchuchumilia moyo wa upendo, mshikamano na
umoja ili wema uweze kuushinda ubaya, kwa kutambua kuwa Mkristo ni mtu mwenye matumaini,
hasa pale anapokabiliana na giza la dunia kutokana na kufanya maamuzi mabaya kinyume
cha imani yake; hata hivyo, mwanga wa Kristo unaweza kuangaza kutoka katika undani
wa maisha yake.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema kwamba,
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani yanapania kumwezesha mwamini kutambua kwamba, kukutana
na Kristo kunamwezesha kupata maana halisi ya maisha na tumaini lisilotetereka. Imani
kwa Kristo inamsukuma mwamini kutenda mema kwa kuondokana na dhambi, ili kuanza maisha
mapya!
Kwa njia ya Fumbo la Umwilisho, mwanadamu ana bahati ya kupata utambulisho,
upendo na changamoto ya kujenga na kuimarisha mshikamano na Kristo. Huu ndio ukweli
mfunuliwa ulioletwa na Yesu unaowamahasisha waamini kuendelea kuwa na tumaini kwa
mwaka mpya wa 2013.
Mama Kanisa amepewa dhamana ya kutangaza Habari Njema ya
Wokovu kwa watu wote, lakini kwa namna ya pekee, vijana wa kizazi kipya wanaoonesha
kiu na njaa ya maana ya maisha, wasiposaidiwa wanaweza kupoteza mwelekeo wa maisha
yao.
Hata mji wa Roma anasema Baba Mtakatifu unapaswa kuinjilishwa na imani
ya Kikristo kutolewa ushuhuda makini, hii ni kutokana na ukweli kwamba, kuna idadi
kubwa ya watu wa dini mbali mbali wanaoishi hapa, kiasi kwamba, inakuwa vigumu hata
kwa Jumuiya za Kiparokia kuweza kuwafikia vijana ambao wanavutwa kwa namna ya pekee
na ubinafsi, mmong'onyoko wa maadili. Kuna kundi la vijana wanaotafuta tumaini lisilodanganya,
kumbe, wanapaswa kusaidiwa na hili ni jukumu la kila mwamini, ili kuamsha ari na moyo
wa kimissionari, mkakati wa kichungaji unaofanyiwa kazi na Kanisa.
Waamini
wanahimizwa kushiriki katika Ibada ya Misa Takatifu; Wazazi na walezi watekeleze wajibu
wa kufundisha na kuwarithisha watoto wao imani, kwani wazazi ndio walezi wa kwanza
wa imani. Waamini waliopokea Sakramenti mbali mbali za Kanisa waendelee kuimarishwa
kwa njia ya majiundo endelevu; tafakari ya Neno la Mungu pamoja na kushirikishana
mang'amuzi ya maisha ya Kikristo katika vyama vya kitume; sanjari na kujenga urafiki
na mshikamano wa dhati; lengo ni kuimarisha maisha ya kiroho, changamoto endelevu
inayotolewa na Mama Kanisa kwa watoto wake.
Baba Mtakatifu anabainisha kwamba,
ili waamini waweze kumtangaza na kumtolea Kristo ushuhuda wa imani yao, hawana budi
kuzifahamu kweli za kiimani, changamoto kwa wadau wa shughuli za kichungaji, kuhakikisha
kwamba, wanatekeleza dhamana yao kwa umakini mkubwa. Waamini waendeleze majadiliano
kwenye Makanisa na wale wote wanaomtafuta Mungu, kweli za Kiinjili na maana ya maisha
yao!
Kanisa Jimboni Roma, halina budi kuwa ni kielelezo cha utajiri wa Injili
ya Kristo; mshikamano na upendo kwa familia ambazo zinakabiliwa na hali ngumu ya maisha
na wale ambao wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha. Ni
matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, taasisi mbali mbali zitawasaidia kupata mahitaji
yao msingi.
Mwishoni Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anahitimisha
mahubiri yake wakati wa Kufunga Mwaka 2012 kwa kusema kwamba, ni fursa ya kushukuru
kwa wema na ukarimu wa Mungu kwa mwaka mpya na kuomba toba na msamaha wa mapungufu
yote ya kibinadamu yaliyojitokeza kwa mwaka uliopita na kwamba, Yesu ndiye utimilifu
wa matumaini ya Kanisa na dunia kwa ujumla.