2013-01-01 09:25:36

Kanisa Katoliki katika mchakato wa kulinda na kutetea haki msingi za binadamu!


Baraza la Kipapa la Haki na Amani tangu kuanzishwa kwake mara tu baada ya maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, limekuwa mstari wa mbele katika kulinda, kusimamia na kutetea haki msingi za binadamu, kama ambavyo zimebainishwa katika Azimio la Haki Msingi za Binadamu, lililotolewa na Umoja wa Mataifa kunako mwaka 1948. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Yohane wa Ishirini na tatu ni kati ya viongozi wa Kanisa Katoliki walioweka bayana umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu zinazojikita katika utu wa binadamu pamoja na uhuru wa kuabudu mintarafu sheria za kimataifa na kitaifa. Hizi ni kanuni msingi zinazobainishwa katika Mafundisho Jamii ya Kanisa, yanayopania kuyatakatifuza malimwengu.

Kwa bahati mbaya anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, haki msingi za binadamu na uhuru wa kuabudu ni kati ya mambo ambayo kwa sasa yako hatarini kutokana na sababu mbali mbali, ndiyo maana kuna haja kwa wadau mbali mbali kusimama kidete kuhakikisha kwamba, haki msingi za binadamu, utu na heshima yake vinalindwa na kudumishwa sehemu mbali mbali za dunia.

Tamko la Haki Msingi za Binadamu la Umoja wa Mataifa ni matokeo ya tafakari ya kina iliyofanywa na viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kuhusu athari zilizokuwa zimesababishwa na vita kuu ya kwanza na ile ya pili ya dunia; ambapo kuna watu wengi walipoteza maisha na mali; utu na heshima yao vikawekwa rehani. Walitaka kuweka kanuni msingi ambazo zimengefuatwa na Jumuiya ya Kimataifa.

Hizi ni haki ambazo zinafumbatwa katika uhuru, haki na amani duniani. Huu ni urithi wa binadamu wa nyakati zote na mahali pote bila ubaguzi, kwani zinapata chimbuko lake kutoka kwa binadamu mwenyewe aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kwamba ni sehemu ya asili ya binadamu.

Ni mchango wa Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani alioutoa hivi karibuni kwenye Kongamano la Kimataifa lililokuwa linajadili kuhusu dhamana ya Kanisa Katoliki katika kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, kwa kutambua kuwa haki hizi zinafumbata utu wa mtu, tangu pale anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake, hadi mauti ya kawaida yanapomsibu kadiri ya mpango wa Mungu.

Tangu mwaka 1948 haki hizi zilipotangazwa na Umoja wa Mataifa, Kanisa limeendelea kuzipigania ili ziweze kutekelezwa na Jumuiya ya Kimataifa na wala zisibaki kwenye makabati tu, kama kumbu kumbu ya nyaraka za kale.

Baba Mtakatifu Yohane wa ishirini na tatu, aliguswa kwa namna ya pekee na kinzani, wasi wasi na woga uliokuwa umetanda wakati wa Vita Baridi sanjari na ujenzi wa Ukuta wa Berlin, Ujerumani, alipoandika Waraka wa Kichungaji, Amani Duniani, Pacem In Terris, akakazia mambo makuu manne kama vigezo vya kudumisha haki msingi za binadamu: amani katika ukweli, haki, upendo na uhuru. Hizi ni tunu ambazo ni urithi mkubwa kwa binadamu wote kwani zinabubujika kutoka katika asili ya binadamu, hivyo zinapaswa kulindwa, kutetewa na kuheshimiwa na wote; kwa kuzingatia kwamba, haki inakwenda sanjari na wajibu; hakuna haki pasi na wajibu.

Hii ni haki ya kuishi, kupata huduma bora ya makazi, afya, elimu, kuabudu, uhuru wa dhamiri, uhuru wa kuchagua mfumo wa maisha; haki za kicuhumi na kisiasa pamoja na uhuru wa kwenda unakotaka kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo.








All the contents on this site are copyrighted ©.