Amani inatoweka duniani kutokana na pengo kubwa kati ya matajiri na maskini; ubinafsi,
kupenda faida kubwa; vitendo vya kigaidi na makosa ya jinai!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Mungu
sanjari na maadhimisho ya Siku ya 49 ya Kuombea Amani Duniani inayoongozwa na kauli
mbiu "heri wapatanishi", ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro, mjini Vatican, kwa kuomba baraka na neema kutoka kwa Neno wa Mungu aliyefanyika
mwili na kukaa kati ya watu wake; changamoto ya kuendelea kusambaza ujumbe wa amani
kati ya Mataifa.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, kinzani, na migogoro ya kisiasa
na kijamii inayoendelea kupamba moto sehemu mbali mbali za dunia, ni matokeo ya uwiano
tenge kati ya matajiri na maskini; watu kugubikwa na ubinafsi; mfumo wa kibepari unaojikita
mno katika faida; vitendo vya kigaidi pamoja na makosa ya jinai. Wajenzi wa amani
ni wengi, wakitekeleza wajibu wao barabara amani inaweza kutawala. Kiu ya amani inakwenda
sanjari na utimilifu wa maisha ya mwanadamu yanayojikita katika furaha ya kweli.
Heri
wapatanishi maana wataitwa wana wa Mungu, kwani amani ni zawadi kutoka kwa Mungu
na kazi ya binadamu. Amani na Mwenyezi Mungu inapatikana kwa kutekeleza mapenzi ya
Mungu; kwa upendo kwa jirani pamoja na utunzaji bora wa mazingira; kazi ya uumbaji.
Ni wajibu wa kila mtu kuitafuta, kujenga na kudumisha amani duniani. Hii ndiyo amani
ya kweli inayopata chimbuko lake kutoka kwa Mwana wa Mungu aliyezaliwa katika hali
duni baada ya kukosa mahali pa kulala mjini Bethelehemu. Bikira Maria anayaweka na
kuyatafakari moyoni mwake matukio yote yanayojionesha wakati wa kuzaliwa kwa Mtoto
Yesu.
Huu ndio utulivu wa ndani, ambao mwanadamu anautafuta katika hija ya
maisha yake, utulivu unaojionesha kwa kutekeleza sheria na mapenzi ya Mungu, kama
alivyofanya Bikira Maria Mama wa Mungu. Yesu ni Mwana wa Mungu, ndiyo maana Kanisa
linamwita Bikira Maria "Mama wa Mungu". Baraka inayotolewa na Mwenyezi Mungu kama
inavyojionesha katika Liturujia ya Neno la Mungu ni kwa ajili ya mafao ya binadamu
na kwamba, amani ni utimilifu wa matendo makuu ya Mungu kwa ajili ya binadamu.
Tafakari
ya uso wa Mungu ni kilele na chemchemi ya furaha, usalama na amani. Ni mwaliko wa
kumfahamu Mwenyezi Mungu kadiri ya uwezo mintarafu ufunuo kutoka kwa Yesu Kristo;
ni kuendelea kulitafakari Fumbo la Umwilisho, ili kufahamu undani wa maisha na kuishi
kadiri ya mpango wake wa upendo kwa mwanadamu sanjari na kujitahidi kumfahamu Mwenyezi
Mungu ambaye ni Baba wa wote!
Baba Mtakatifu anasema, msingi wa amani ni tafakari
ya kina kuhusu Yesu Kristo pamoja na kuangaziwa ile sura ya Mwenyezi Mungu kwa waamini
kutambua kwamba, wao ni watoto wa Mungu, chemchemi ya amani inayojikita kwa Emmanuel,
yaani Mungu pamoja nasi. Ni amani ambayo inafumbatwa katika imani na neema. Hakuna
jambo lolote ambalo linaloweza kuiondoa amani hii na kwamba, mateso na mahangaiko
yanasaidia kukuza matumaini ambayo kamwe hayawezi kudanganya, kwani upendo wa Mungu
umekwisha kumiminwa mioyoni mwa waamini kwa njia ya Roho Mtakatifu.
Baba Mtakatifu
anahitimisha mahubiri yake katika Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Mungu sanjari na
Maadhimisho ya Siku ya 49 ya Kuombea Amani Duniani kwa kumwomba Bikira Maria awasaidie
waamini kuutafakari uso wa Yesu, Mfalme wa Amani. Awasaidie na kuwasindikiza katika
hija ya Mwaka Mpya 2013 pamoja na kuwakirimia zawadi ya amani.