2012-12-31 08:10:11

Yesu Kristo Mfalme wa Amani awajalie watu wa mataifa kushinda kishawishi cha chuki, uhasama, magovi na kukumbatia misingi ya haki, amani na upendo wa kidugu!


Kanisa katika kipindi hiki cha Noeli linaendelea kusali kwa ajili ya kuombea haki na amani huko Mashariki ya Kati kutokana na hali ngumu ya maisha: kisiasa, kidini na kijamii, changamoto kwa waamini wa dini na madhehebu mbali mbali, kushiriki katika ujenzi wa misingi ya haki na amani ambayo ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, lakini inapaswa kudumishwa na wanadamu.

Kanisa linamwomba Mtoto Yesu aliyezaliwa kati ya maskini na wadhambi: awasaidie na kuwafariji wote wanaoteseka kiroho na kimwili na kwamba, watu wadhamirie kuanza mchakato wa uejnzi wa tunu ya msamaha, ukweli na upatanisho. Siku kuu ya Noeli, ni mwanzo wa Habari Njema ya Wokovu inayoletwa na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia.

Ni maneno yaliyotolewa na Patriaki Fouad Twal wa Yerusalem wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli mjini Bethlehemu alikozaliwa Yesu. Fumbo la Umwilisho, linapata utimilifu wake katika maadhimisho ya Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Ni Fumbo ambalo ni kielelezo makini cha utimilifu wa kazi ay uumbaji na ukombozi inayoletwa na Yesu Kristo.

Mtoto Yesu amezaliwa kwa ajili ya maskini na wadhambi; wanaoteswa na kusukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na imani na hali yao ya maisha: Yesu ni kwa ajili ya wote ambao bado hawajapoteza matumaini yao kwa Mwenyezi Mungu. Anamkirimia na kumrudishia mwanadamu utu na heshima ya kuitwa tena mwana mpendwa wa Mungu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Hii ndiyo ile sura iliyokuwa imechakaa kutokana na uwepo wa dhambi. Yesu Mwana wa Mungu anakuja ulimwenguni kutangaza sheria mpya inayosimikwa katika upendo kwa Mungu na jirani.

Ni kielelezo makini cha matumaini yasiyodanganya kamwe na mwaliko wa kuendeleza ule mchakato unaowaunganisha wote ili waweze kujisikia kuwa ni ndugu wamoja kwani wameumbwa na Mwenyezi Mungu, tofauti zao za kidini, kitamaduni, kisiasa na kiuchumi ni utajiri kwa ajili ya kusaidiana kwa hali na mali na wala hazipaswi kuwa ni chanzo cha kinzani na migogoro ya kisiasa, kijamii na kidini.

Yesu amekuja ulimwengu ili kuipatanisha mbingu na dunia ambayo imempokea na kumpatia fursa ya kuishi kama binadamu katika mambo yote isipokuwa dhambi. Ni chachu ya upatanisho kati ya mwanadamu na Muumba wake na kati ya binadamu na jirani yake.

Ameleta mageuzi kwa wale waliokuwa wanadhaniana adui, waweze kujivika utu mpya na kuanza kushirikishana kama marafiki na wenza katika hija ya maisha ya hapa duniani. Ikumbukwe kwamba, chuki, uhasama, magomvi na vita ni kazi ya shetani, lakini waamini wa dini mbali mbali wanaweza kushinda kishawishi hiki kwa kukumbatia misingi ya haki, amani,upendo na mshikamano wa kidugu!








All the contents on this site are copyrighted ©.