2012-12-31 08:05:22

Waamini wasaidie mchakato wa binadamu kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani yake!


Wakristo wanahamasishwa kuwa ni vyombo vya kuleta mabadiliko katika Jamii, kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili na matakatifu, katika ulimwengu huu ambao umekuwa kama tambarabovu. Ili kukabiliana na changamoto zote hizi, Wakristo hawana budi kujishikamanisha na Yesu Kristo, aliyekuja ulimwenguni ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti, na hivyo, kumkirimia mabadiliko makubwa katika hija ya maisha yake hapa duniani. Wakristo wanaweza kusaidia mchakato wa mwanadamu kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani yake.

Ni maneno ya Askofu mkuu Dr. Rowan Williams wa Jimbo kuu la Cantebury, ambaye pia ni kiongozi mkuu wa Jumuiya ya Waanglikani Duniani, wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli. Ili kuleta mabadiliko ya kweli, kuna haja kwanza kwa waamini wenyewe kuchunguza dhamiri zao katika kioo cha ukweli na uwazi mbele ya Mwenyezi Mungu; kwa kutambua na kuthamini wajibu na dhamana ambayo kila mwamini amekabidhiwa na Jamii husika.

Wakristo wasikatishwe tamaa na magumu, changamoto na kinzani mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika safari ya maisha yao hapa duniani. Wajishikamanishe na watu wengine, wakitambua wajibu na dhamana yao ya kuwa ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa. Hii ndiyo changamoto kubwa inayoonesha ushupavu na ushujaa wa kikristo unaojikita katika wito wa Kristo: tubuni na kuiamini Injili ili muweze kubatizwa.

Maadhimisho haya ya Noeli kwa Mwaka 2012 yamekuwa ni ya mwisho kwa Askofu mkuu Rowan Williams ambaye baada ya muda si mrefu atang’atuka kutoka madarakani na kumwachia mrithi wake Askofu mkuu Justin Welby wa Jimbo Durham anayetarajiwa kusimikwa rasmi hapo tarehe 21 Machi 2013.

Wakati wa mahubiri yake, Askofu mkuu Williams amegusia kwamba, wajumbe wa mkutano mkuu wa Kanisa Anglikani uliohitimishwa hivi karibuni wamekataa kuridhia pendekezo la kuwaweka wakfu wanawake ili kuwa Maaskofu wa Kanisa Anglikani, jambo ambalo linaendelea kuwa ni kizingiti katika mchakato unaopania kudumisha na kuimarisha umoja na mshikamano miongoni mwa waamini wa Kanisa Anglikani na Wakristo wengine katika ujumla wao.








All the contents on this site are copyrighted ©.