2012-12-31 08:24:06

Mwaka wa Imani uimarishe toba na wongofu wa ndani, ili kuchuchumilia utakatifu wa maisha!


Maadhimisho wa Mwaka wa Imani ni changamoto na mwaliko kwa Familia ya Mungu sehemu mbali mbali za dunia kujikita zaidi katika maisha ya sala, toba na wongofu wa ndani, kama kielelezo makini cha kuchuchumilia utakatifu wa maisha. Wongofu wa ndani, unajikita katika maisha ya sala. Ni changamoto inayotolewa na Askofu John Buckely wa Jimbo Katoliki Cork na Ross nchini Ireland. RealAudioMP3

Familia ya Mungu inaweza kuchuchumilia toba na wongofu wa ndani kwa njia ya kujikita katika Tafakari ya kina ya Neno la Mungu, linalomwilishwa katika uhasilia wa maisha ya waamini. Ni mwaliko wa kujikita kusali kwa pamoja kwa kuanzia katika: Familia, Jumuiya Ndogo ndogo na Vyama vya Kitume, kwa pamoja wakipania kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu, linalowawezesha kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani zao. Yesu Kristo, muasisi wa Kanisa nyakati zote za historia ya Kanisa ameendelea kuibua watakatifu na wafiadini kwa nyakati mbali mbali ili kuwa kweli ni kielelezo cha toba, wongofu wa ndani na utakatifu wa maisha.

Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ni mwaliko na changamoto ya kuchuchumilia toba na wongofu wa ndani na kwamba, huu ni wito na mwaliko kwa kila mwamini na wale si kwa ajili ya upendeleo wa watu wachache. Utakatifu upate chimbuko lake katika maisha ya sala na imani tendaji, kwa kuomba ulinzi wa daima kutoka kwa Bikira Maria, Mwanamke wa Imani aliyeonesha imani yake katika matendo kwa kuukubali Mpango wa Mungu katika maisha yake, akawa tayari kuwashirikisha jirani zake, ile furaha ya kuwa Mama wa Mungu, Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili.

Askofu John Buckley kutoka Ireland anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuwashirikisha wengine ile furaha ya kugundua tena imani yao, wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani; ili watu wengi zaidi waweze kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Yesu Kristo; kwa kutekeleza dhamana na wajibu waliojitwalia wakati walipopokea Sakramenti ya Ubatizo.

Itakumbukwa kwamba, Mwaka wa Imani uliozinduliwa rasmi na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita hapo tarehe 11 Oktoba 2012 utahitimishwa rasmi hapo tarehe 24 Novemba 2013, Katika Maadhimisho ya Sherehe ya Kristo Mfalme.










All the contents on this site are copyrighted ©.