2012-12-31 10:40:33

Kuna magenge ya vijana wasiokuwa na fursa za ajira Zanzibar yanatumiwa kuhujumu misingi ya haki, amani na mshikamano wa kitaifa Visiwani Zanzibar!


Askofu Augustino Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar, wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, amezungumzia tatizo la kukithiri kwa biashara haramu ya dawa za kulevya inayosababisha madhara makubwa kwa Jamii visiwani Zanzibar na kwamba, umefika wakati kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuwafichua na hatimaye, kuwachukulia hatua za kisheria. Serikali iwavalie njuga wafanyabiashara wakubwa ili kukata mzizi wa biashara hii haramu inayoendelea kusababisha madhara makubwa kwa wananchi Zanzibar.

Jamii iwajibike kuwasaidia wathirika wa matumizi haramu ya dawa za kulevya, ambao wanajikuta wametumbukia huko kutokana na umaskini pamoja na sababu mbali mbali za maisha. Kuna kundi kubwa la vijana Visiwani Zanzibar ambalo halina fursa za ajira, linaishi katika mazingira hatarishi na matokeo yake ni kujitumbukiza katika matumizi haramu ya dawa za kulevya na ukahaba; mambo ambayo pia yanachangia kuongezeka kwa maambukizi ya Virusi vya Ukimwi na makosa ya jinai.

Kundi hili limeanza kutumiwa na baadhi ya wanasiasa na viongozi wa kidini wanaotumia vijana hawa wasiokuwa na ajira kwa malengo binafsi. Ghasia na uchomaji wa Makanisa Visiwani Zanzibar chini ya mwamvuli wa kupinga muungano ni dhana nyemelezi ya wenye madaraka nje na ndani ya Visiwa vya Zanzibar kutaka kutumia umaskini wa vijana kuhataraisha amani, umoja na mshikamano wa kitaifa. Askofu Shao anawahimiza vijana kukataa katu katu kutumiwa kwa misingi ya dini, itikadi za kisiasa na kiuchumi kwa manufaa ya watu binafsi.

Wananchi wanatakiwa kutoa maoni yao kuhusu Katiba Mpya itakaozingatia mafao ya wengi, uhuru wa kuabudu pamoja na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Wakati huo huo habari kutoka Zanzibar zinabainisha kwamba, Jeshi la Polisi limewatia watu wawili mbaroni kwa kuhusishwa na tuhuma za kumshambulia kwa risasi Padre Ambrose Mkenda wa Jimbo Katoliki Zanzibar. Watu hao wanaendelea kuhojiwa na Polisi ili kuwapata watu wengine walioshiriki katika kupanga na kutekeleza njama ya kuvamia na kumjeruhi Padre Mkenda kwa risasi, tukio ambalo limevuta hisia kubwa ndani na nje ya Tanzania. Inasemekana kuna genge la watu ambalo limekuwa likifanya hujuma dhidi ya viongozi wa kidini na watu wasiokuwa na hatia Visiwani Zanzibar wanaosimama kidete kutangaza haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Padre Ambrose Mkenda mwenye umri wa miaka hamsini na mbili, Paroko wa Parokia ya Mpendae amekuwepo Zanzibar tangu mwaka 1995 na ameendelea na utume wake bila shida wala wasi wasi. Anasema, kuna haja sasa kwa Serikali kuchukua hatua kali zaidi kwa watu wanaochezea na kutaka kuhatarisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa Visiwani Zanzibar. Hii ni dhamana inayopaswa kufanyiwa kazi ndani ya Familia na Jamii katika ujumla wake, ili kupata kizazi cha watu wanaoheshimihana na kuthaminiana kamka ndugu.

Takwimu zinaonesha kwamba, kuanzia mwaka 2001 hadi kufikia mwaka 2012 jumla ya Makanisa 25 pamoja na baa 12 zilichomwa moto na "watu wasiojulikana". Hadi sasa hakuna taarifa rasmi zinazoonesha kwamba, watu hawa wametiwa mbaroni na wanatakiwa kujibu tuhuma zinazowakabili.

Padre Ambrose Mkenda alipigwa risasi shingoni tarehe 25 Desemba 2012 majira ya saa 1: 45 katika eneo la Tomondo. Akafanyiwa operesheni ili kuondoa risasi zilizokuwa mwilini mwake hapo Ijumaa tarehe 28 Desemba 2012, kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Tangu wakati huo viongozi waandamizi kutoka Serikalini wamemtembelea Padre Mkenda ili kumtakia hali. Kati yao ni Rais Jakaya Kikwete, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi,Makamu wa Rais Dr. Mohammed Gharib Bilal; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud Mohammed. Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamini William Mkapa naye amemtembelea Padre Ambrose Mkenda. Wapenda haki na amani wanafuatlia kwa umakini mkubwa mkasa huu ambao umeibua hisia tofauti kuhusu haki, amani na mshikamano wa kitaifa Visiwani Zanzibar.







All the contents on this site are copyrighted ©.