2012-12-29 14:03:53

Askofu mkuu Rugambwa aanza ziara ya kichungaji nchini Siera Leone


Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa kuanzia tarehe 31 Desemba 2012 hadi tarehe 7 Januari 2013 atakuwa na ziara ya kichungaji nchini Siera Leone ili kumweka wakfu na hatimaye kumsimika Askofu mteule Henry Aruna wa Jimbo Katoliki Makeni.

Askofu mkuu Rugambwa, akiwa nchini Siera Leone, hapo tarehe 5 Januari 2013 anatarajiwa kukutana na Baraza la Maaskofu Katoliki Siera Leone pamoja na Makleri wa Jimbo Katoliki Makeni. Atatembelea Seminari kuu Mtakatifu Paulo iliyoko Mjini Freetown pamoja na kukagua miradi inayofadhiliwa na Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa.

Kwa takribani miaka ishirini na mitano, Jimbo Katoliki Makeni liliongozwa na Askofu George Biguzzi. Takwimu zinaonesha kwamba, waamini wa Jimbo Katoliki Makeni ni zaidi ya 50, 000, sehemu kubwa ya wakazi wa Makeni ni waamini wa dini ya Kiislam. Jimbo lina jumla ya Parokia kumi na mbili zinazohudumiwa na Mapadre wa Jimbo 32 na Mapadre wa Mashirika ya kitawa ni 34. Kuna Mapadre wa Fidei Donum 4. Jimbo lina jumla ya Makatekista 156. Lina taasisi za elimu katika ngazi mbali mbali zipatazo 219 na taasisi za huduma ni 9.

Askofu mteule Henry Aruna wa Jimbo Katoliki Makeni alizaliwa tarehe 2 Agosti 1964. Akapadrishwa tarehe 16 Aprili 1992. Tarehe 7 Januari 2012, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, akamteua kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Makeni, Siera Leone.







All the contents on this site are copyrighted ©.