Familia ni kitovu cha utume wa Kanisa katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya
Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria linabainisha kwamba familia ni kitovu cha utume
wa Kanisa katika Uinjilishaji Mpya. Kwa kuinjilisha familia, Jamii nzima itakuwa imeinjilishwa.
Hayo yamesemwa na Askofu Hilary Okeke wa Jimbo Katoliki la Nnewi, Nigeria, wakati
akifungua mkutano mkuu wa Chama cha Wanasheria za Kanisa nchini Nigeria, uliokuwa
unaongozwa na kauli mbiu “ Shughuli za kichungaji kwa ajili ya Familia: utume
na changamoto zake.
Familia
ni kati ya taasisi ambazo zinakabiliwa na changamoto nyingi katika ulimwengu wa utandawazi
na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Ndoa na familia za Kikristo zinapaswa kusimama
kidete, vinginevyo zinaweza kumezwa na malimwengu kutokana na Jamii kukengeuka. Uinjilishaji
Mpya hauna budi kufanyika kwa kutoa kipaumbele kwa Familia ambayo ni urithi wa kila
mwanadamu na matumaini ya kesho iliyo bora zaidi.
Hapa ni mahali ambapo wanafamilia
wanajifunza kupenda na kupendwa, kusamehe na kusamehewa; kupokea na kutoa kwa njia
ya ukarimu. Familia ni shule ya kwanza kabisa inayorithisha tunu msingi za maisha
ya kiroho, kiutu na kitamaduni. Watoto wana uwezo wa kupokea kile kinachotolewa na
wazazi pamoja na walezi wao, kumbe, wazazi na walezi wanapaswa kuwa kweli ni mifano
bora ya kuigwa kwa maneno na matendo yao!
Askofu Okeke anawaalika Wanasheria
wa Kanisa kuhakikisha kwamba, wanajenga na kuimarisha utakatifu na tunu msingi za
maisha ya kifamilia mintarafu Mafundisho Tanzu ya Kanisa kuhusu ndoa na familia.
Wajumbe
wa mkutano huu wamekazia umuhimu wa mafunzo ya awali na endelevu kwa wanandoa watarajiwa,
ili waweze kutambua na kuthamini ndoa ya Kikristo ambayo ni ya kudumu hadi kifo kitakapowatenganisha
kadiri ya mpango wa Mungu. Wanandoa watarajiwa waepukane na uchumba sugu unaowanyima
kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.
Askofu Okeke alionesha
masikitiko yake kutokana na athari zinazojitokeza kwenye ndoa za wake wengi, zinazoendelea
kumdhalilisha mwanamke na kumfanya kuwa ni chombo tu cha kukidhi tamaa ya mwili. Kanisa
Barani Afrika halina budi kujitahidi kuhakikisha kwamba, linaonesha uzuri wa maisha
ya ndoa na familia kwa kuzingatia mila na desturi nzuri za Kiafrika.
Watu
hawana budi kuachana na mila na desturi zilizopitwa na wakati, ili kukuza na kudumisha
upendo wa dhati; umoja na mshikamano; amani na utulivu. Wanawake waheshimiwe na kuthaminiwa
utu na nafasi yao katika maisha ya ndoa na familia na wala si vichokoo vya kukidhi
matamanio ya wanaume. Ndoa za wake wengi ni kielelezo cha unyanyasaji wa kijinsia,
dhuluma, kinzani na migawanyiko, kinyume kabisa na utamaduni wa upendo wa dhati ambao
Mwenyezi Mungu aliudhamiria kwa ajili ya mwanadamu tangu kuumbwa kwake na Kristo akautakatifuza
kwa kuweka Sakramenti ya ndoa kati ya Bwana na Bibi.
Uhuru usiokuwa na mipaka
na watu kupenda kujitawala bila kuwajibika, kumepelekea ongezeko kubwa la talaka na
baadhi ya watu kukumbatia utamaduni wa kuenzi “vidumu” au nyumba ndogo kama zinavyojulikana
kwa Waswahili wengi.
Lakini jambo la kushangaza ni kule kukengeuka kwa watu
kimaadili kiasi kwamba, watu wa jinsia moja wanataka kufunga ndoa, jambo ambalo linapigiwa
debe na baadhi ya nchi za Magharibi, kiasi hata cha kutishia kuchomoa misaada kwa
nchi zile ambazo hazitaridhia sheria eti kama kielelezo cha uhuru na haki sawa. Huu
ni utamaduni wa kifo unaosigana na mpango wa Mungu katika kazi ya uumbaji.
Kanisa
lazima lisimame kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya ndoa na familia,
kwa kuheshimu na kutunza mila na tamaduni njema za kiafrika badala ya kugenishwa na
mambo yanayopelekea kumong’onyoka kwa maadili na utu wema. Ndoa ya Kikristo inajengeka
katika msingi wa Bwana na Bibi, wakipania kupata watoto ambao ni zawadi kutoka kwa
Mwenyezi Mungu. Ni agano la kudumu kati ya watu wawili wanaopendana na kushibana kwa
dhati bila shuruti.
Kanisa kwa njia ya Katekesi ya kina, Sheria na Kanuni za
maisha ya ndoa linapenda kulinda na kutunza tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.
Ni dhamana kwa viongozi wa Kanisa kuhakikisha kwamba, wanaonesha utakatifu wa maisha
katika ndoa na wala si tendo la watu kuishi kwa pamoja tu! Hii ni Sakramenti, chemchemi
ya neema na utakaso, inayowawezesha wanandoa kusaidiana katika hija ya maisha yao
ya kila siku, ili hatimaye, kufikia utakatifu.
Familia haina budi kuwa ni
shule ya kwanza ya tunu msingi za kiroho na maisha adili; ioneshe utakatifu wa maisha
mintarafu upendo wa Kristo kwa Kanisa lake. Waamini wachangamotishwe kupenda na kuthamini
tunu msingi za maisha ya ndoa na familia za Kikristo, kamwe wasimezwe na malimwengu,
huko watapotea!