2012-12-27 09:05:49

Familia na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia!


Mara nyingi ninapotafakari neno familia mawazo yangu yanavutwa kutafakari mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Tunapotafari kuhusu familia tuyapeleke mawazo yetu kwa baba, mama na watoto kama ilivyokuwa katika Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. RealAudioMP3

Familia Takatifu inatukumbusha mwaliko wetu wa kuwa watakatifu; na familia inapewa heshima kubwa ya kuwa ni shule ya kwanza ya utakatifu. Tukitafakari Fumbo la Mungu kujifanya mwanadamu, tunaweza kujiuliza maswali mengi na swali mojawapo ni kwanini Mungu aliamua kushuka kwetu kwa kupitia njia ya familia? Kutokana na uwezo wake angeweza kuja kwa njia nyingine yeyote ambayo angependelea.

Lakini, mpango wa Mungu kujifanya mtu kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, kuzaliwa kama binadumu wa hali ya chini na kuishi kama sisi binadamu akiwa sawa katika mambo yote isipokuwa dhambi, ni kutualika sisi wote tuweze kuwa kama yeye, maana yake tuweze kuwa watakatifu na utakatifu huo anatuonesha kuwa unaanzia katika familia zetu.

Bwana wetu Yesu Kristo anatuonesha njia pekee yenye kuleta mafanikio katika maisha ya familia ni: unyenyekevu kwa Mungu na kunyenyekeana wenyewe kwa wenyewe. Kristo na Umungu wake alijinyenyekesha na kuzaliwa na Bikira Maria, akawa ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu. Bikira Maria na Yosefu walikuwa wanyenyekevu kupokea mapenzi ya Mungu katika maisha yao na pia walinyenyekeana wao kwa wao.

Bila mume na mke kuwa wanyenyekevu kwa Mungu yaani kupokea Neno la Mungu na kufuata maongozi yake kupitia Kanisa lake takatifu, na bila mume kuwa mnenyekevu kwa mke na mke kuwa mnyenyekevu kwa mume katika kutimza dhamana na majukumu ya kila siku familia hawezi kusimama imara.

Mume na mke wanapoamua kuishi pamoja kama mume na mke wanapokea mwaliko wa kuwa watakatifu na kuwasaidia watoto watakaojaliwa kama zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kuupata utakatifu. Kazi ya kwanza ni kusaidiana wenyewe kama mume na mke kuwa watakatifu; kazi ya pili ni kuwasaidia watoto wao kuwa watakatifu na kazi ya tatu ni kuwa mwanga na chumvi kwa taifa zima la Mungu kwa mifano bora na tunu msingi za maisha ya kifamilia.

Katika ulimwengu wetu, kuna mambo mengi ambayo yanaweza kuhatarisha zawadi kubwa ya maisha ya familia. Kwa leo ningependa tutafakari pamoja changamoto moja kuhusu tatizo la uchumba sugu katika jamii zetu. Ninapozungumzia uchumba sugu: ninamaanisha mume na mke kuamua kuishi pamoja kwa muda mrefu bila kuomba Baraka za Mungu katika Sakramenti ya Ndoa. Matokeo yake tunashindwa kuweka mahusiano yetu wazi mbele ya Mungu na taifa zima la Mungu, na kumwomba Mwenyezi Mungu abariki uhusiano huo na kutujalia neema ya kuishi agano tunalo mwahidia katika msingi wa Ndoa Takatifu.

Mara nyingi “wapenzi wawili” wanapokutana na kutaka kuishi pamoja wanatumia neno upendo “ninakupenda”, lakini wakisha amua kushi pamoja wanasema kwamba “tunapimana”. Kama tunasubiri mpaka tuwe watakatifu ndipo tuweze kuweka agano la ndoa hali hiyo haiwezekani katika ulimwengu huu. Maisha ya kutafuta utakatifu ni mapambano ya kila siku katika maisha yetu.

Neno linalotumika mwanzoni watu wanavyoanza kutafutana “ninakupenda”, katika lugha ya kibinadamu ni sawasawa kwasababu mara nyingi binadamu tunatawaliwa na vionjo, lakini, neno hilo linahitaji kukamilishwa na upendo wa Kimungu. Hivyo basi hii hali ya vionjo vya kibinadamu katika kupenda inapokamilishwa na upendo wa kimungu inatengeneza mapendo ya kweli kati ya mume na mke. Mtu hawezi kuwa na upendo wa kimungu ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu kama hajajaliwa na Mungu mwenyewe.

Zawadi ya upendo wa Kimungu tunajaliwa tunapokuwa na ushirikiano mzuri na Mungu katika maisha yetu ya kila siku, yaani Kusoma na kutafari Neno la Mungu mara kwa mara katika maisha yetu na kuwa tayari kupokea wajibu tunaopewa na Neno hilo; kushiriki kiaminifu katika Sakramenti za Kanisa hususani Sakramenti ya Kitubio na Ekaristi Takatifu; kuishi maisha ya Sala na kumkabidhi Mungu awe kiongozi mkuu wa maisha yetu.

Dalili ya upendo wa Kimungu katika familia inadhihirishwa na mtu kujitoa kwa mwenzake kama alivyo na kumpokea mwenzake kama alivyo; yaani: katika mazuri na mapungufu, na kusaidiana kwa pamoja kwa msaada wa Mungu kuboresha yale mazuri na kurekebisha yale mapungufu; maana yake: kusaidiana katikaka kuutafuta utakatifu.

Sote tunaalikwa kutafuta utakatifu kila siku ya maisha yetu hapa duniani. Yesu mwenyewe anatueleza wazi ya kuwa “mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake wa kila siku, anifuate”(LK 9:23). Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanabainisha kwamba, utakatifu ni wito na mwaliko kwa kila mfuasi wa Kristo na wala si fursa kwa watu wachache ndani ya Kanisa, kama alivyokazia Mwenyeheri Mama Theresa wa Calcutta.
Kutoka Studio za Radio Vatican, mimi ni Shemasi Titus Nkane, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.