Wekezeni katika elimu kama njia ya kumkomboa mwanadamu: kiroho na kimwili!
Askofu Godrey Mdimi Mhogolo wa Kanisa Anglikani, Dayosisi ya Kati, anawataka watanzania
kuenzi Fumbo la Umwilisho kwa kuwekeza katika sekta ya elimu ambayo ni dira na msingi
wa maendeleo ya mtu kiroho na kimwili. Kuna umuhimu wa kujenga na kuimarisha msingi
wa elimu bora kwa ajili ya maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili; sanjari na mapambano
dhidi ya baa la umaskini unaowakabili Watanzania na Taifa kwa ujumla.
Askofu
Mhogolo ameyasema hayo wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, iliyofanyika kwenye
Kanisa kuu la Roho Mtakatifu, Dodoma. Kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia,
kunapania kumletea mwanadamu ukombozi wa kweli kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Ni changamoto kwa watanzania kujifunga kibwebwe kufanya kazi kwa bidii, juhudi na
maarifa.
Ni jukumu lao kulinda, kutetea na kudumisha amani kwa njia ya elimu
inayojikita katika: upendo, mshikamano, ukweli, msamaha na upatanisho. Toba na wongofu
wa ndani iwasaidie watanzania kuondokana na mambo yanayosigana na maadili na utu wema
kama vile: rushwa, ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma. Kutokana na watu kutafuta
mali kwa nguvu sana, wanajikuta wakipokonya haki msingi za watu wengine ndani ya Jamii,
jambo ambalo ni hatari sana.
Wakristo wamekuwa mstari wa mbele kuwekeza katika
sekta ya elimu nchini Tanzania, kwani kati ya Vyuo 19 vilivyoko nchini Tanzania, vyuo
7 vinamilikiwa na kuendeshwa na Wakristo, Vyuo 11 vinamilikiwa na Serikali na Waamini
wa dini ya Kiislam Tanzania wanaendesha chuo kikuu kimoja! Dodoma imeaanza kubadilika
na kuboreka kutokana na uwepo wa Vyuo vikuu na taasisi nyingi za elimu ya juu.
Anawataka
wananchi wa Dodoma kutokatishwa tamaa na hali ya hewa na historia iliyokuwepo tangu
awali, kwani Mungu amemkirimia mwanadamu akili na ufahamu, ana uwezo wa kufanya mabadiliko
makubwa katika maisha yake. Ni changamoto ya kujipanga upya, kwani kila jambo linawezekana
kwa msaada wa Mungu.
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Amani Karume ni kati
ya watanzania wanaopaswa kuendelea kuenziwa kutokana na mchango wao mkubwa kwa maendeleo
na ustawi wa watanzania wote; ni kielelezo cha: uhuru, amani, umoja na mshikamano
wa kitaifa; walikuwa ni kimbilio la watu waliokuwa na shida kutoka ndani na nje ya
Tanzania. Viongozi hawa ni mfano bora wa kuigwa na Jamii ya watanzania, ili kusonga
mbele kwa imani na matumaini makubwa!