Noeli ni kipindi cha amani, upendo na mshikamano na wala si wakati wa kutopea katika
dhambi!
Mke wa Waziri Mkuu wa Tanzania, Mama Tunu Pinda amesema kila mtu hana budi kumshukuru
Mungu kwa kumfikisha salama wakati wa sikukuu ya Noeli kwani kuna wengine ambao walitamani
kuiona siku hii lakini wameshindwa.
Ametoa kauli hiyo leo Jumanne, Desemba
25, 2012 mara baada ya Ibada ya Noeli iliyofanyika katika kigango cha Kibaoni, Jimbo
Katoliki la Mpanda, Tanzania. “Tunapaswa kumshukuru Mungu kwa kutuwezesha kufika sikukuu
hii, mpaka leo ni mapenzi yake hakuna binadamu ambaye ana amri na maisha yake. Tutakumbuka
hata mwaka jana tulikuwa na Askofu wetu wa Jimbo la Mpanda lakini leo hii hatunaye,
hivyo sote tunapaswa kumshukuru Mungu kwa kutupa uhai,” alisema.
Alisema katika
kuadhimisha sikukuu hii watu hawana budi kuwa na kiasi, wasinywe sana hadi kusababisha
magomvi. Aliwasihi wazazi wawe karibu na familia zao, na wawajibike kwao. ”Tumuombe
Mungu atupe neema, yale tuliyokosea mwaka 2012 tuyaache, tujiandae kuingia mwaka 2013
na yale mazuri tuliyoyaona mwaka 2012,” alisema.
Naye Padre John Giji wa Shirika
la Wamisionari wa Mt. Thomas ambaye aliongoza ibada hiyo, aliwataka waumini wa kigango
hicho kuwajali wenye shida na siyo kujiingiza katika matendo mabaya wakati wa sikukuu.
“Kuishi
kwetu kuanzia leo lazima kuwe na mabadiliko, ni lazima tuwajali wenzetu katika shida
zao kwani kwa kufanya hivyo, tutakuwa na mabadiliko ya kiroho na hivyo kuweza kukua
kiimani,” alisema Padre John ambaye pia ni Paroko wa Usevya.
“Wako watu wanasherehekea
Krismasi kwa matendo mabaya kama vile uzinzi na ujambazi. Huo siyo ukristo tunaotegemewa
kuwa nao katika familia takatifu ya Mungu. Tukifanya kazi kwa bidii, hatuwezi kuwa
na tamaa ya vitu vya wengine,” alionya. “Leo ni sikukuu, tufurahi kwa amani bila jazba
za kidunia. Tusherehekee kwa upendo na amani, ” alisisitiza.