Mashambulizi ya kijeshi yana athari kubwa kwa maisha ya watu na mali zao! Kuzeni utamaduni
wa majadiliano, upendo na mshikamano!
Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki,
Cor Unum anasema, ni matumaini ya Kanisa kwamba, Jumuiya ya Kimataifa haitarudia tena
makosa ya kufanya mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Syria, kama ilivyojitokeza nchini
Iraq, Libia na Pwani ya Pembe kama suluhu ya kinzani na migogoro ya kivita iliyokuwa
inaendelea katika nchi hizi.
Kardinali Sarah anasema, hija yake ya kichungaji
aliyoifanya hivi karibuni nchini Lebanon kwa niaba ya Baba Mtakatifu Benedikto wa
kumi na sita, inaonesha kwamba, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutekeleza kwa
vitendo maamuzi yao na waamini kwa upande wao wanapaswa kuendelea kutekeleza wajibu
wao wa kusali ili kuombea amani na utulivu katika nchi zao kwani amani, kimsingi ni
zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayotoa dhamana kwa binadamu kuendelea kuifanyia
kazi.
Kardinali Sarah ameyasema haya mara tu baada ya Maadhimisho ya Siku kuu
ya Noeli kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, wakati Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, alipomaliza kutoa ujumbe wake kwa mji wa Roma na Dunia kwa ujumla,
unaojulikana kwa lugha ya Kilatini "Uribi et Orbi". Baba Mtakatifu amekazia pamoja
na mambo mengine umuhimu wa Jumuiya ya Kimataifa kujikita katika misingi ya haki,
amani, upendo na upatanisho wa kweli. Vita na mashambulizi yana athari kubwa kwa maisha
na mali ya watu.
Umefika wakati anasema Kardinali Robert Sarah kwa Jumuiya
ya Kimataifa kujenga utamaduni wa majadiliano ya kweli na kina! kama njia ya kutafuta
suluhu ya kinzani, migogoro na vita inayoendelea kuibuka sehemu mbali mbali za dunia,
kama alivyobainisha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika ujumbe wake wakati
wa Noeli.
Dunia imechoka kusikia mtutu wa bunduki ukirindima, ni maneno yaliyosemwa
na Papa Paulo wa sita, yapata miaka hamsini iliyopita, yanaendelewa kurudiwa tena
na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwani watu wanatamani kuona amani, usalama
na utulivu vikitawala katika mioyo na kwenye viunga vya miji na vitongoji vyao.
Mama
Kanisa hatakaa kimya na kuangalia vita ikiendelea kutokea sehemu mbali mbali za dunia,
anawaalika waamini na wote wenye mapenzi mema anasema Kardinali Robert Sarah kuombea
amani sanjari na kuendelea kusaidia wale wanaoathirika kutokana na migogoro ya kivita
na kinzani za kijamii, kwani upendo na mshikamano wa dhati ni sehemu ya vinasaba vya
Watoto wa Kanisa.