2012-12-24 11:36:59

Siku kuu ya Noeli itusaidie kutafakari kuhus: Imani, Matumaini na Mapendo ya Mungu kwa binadamu!


Waamini wapenzi, Tumsifu Yesu Kristo! RealAudioMP3

Ndugu zangu ni Noeli. Fumbo kuu la Noeli liko katika maneno haya“Neno akatwaa mwili na kujenga hema yake kati yetu!” Sikukuu ya leo ni kilele cha tafakari ya Kanisa juu ya fumbo hilo la Noeli.

Noeli, ni sikukuu inayojulikana sana ulimwengu, na karibu imechukua sura ya kiutamaduni zaidi kuliko ile ya kikristu. Siku ya noeli imekuwa ni sikukuu ya kujimwaga kwenye maraharaha na hasa kwenye uchumi. Sisi tunaosadiki bado katika mtoto huyu aliyezaliwa maskini na kwenye mazingira ya kimaskini, leo tunaalikwa kumkaribisha mioyoni mwetu, aweze kupata makao, kumbembeleza, kumshangaa, kumfurahia na kumwabudu.

Tuwe na imani hai, matumaini halisi, na upendo mkubwa wa kuweza kumkaribisha Yesu anayekuja. Tuingine katika fumbo la Noeli kwa hisia ya imani, matumaini na upendo ili mioyo yetu iweze kupanuka na kumwachia nafasi kubwa ya kuingia mtoto anayefika, pasipo sisi kuchanganyikiwa na mianga mingine ya uwongo na sauti danganyifu za ulimwengu wetu wa leo.

1. Kuwa na imani:

Tunatambua kwamba katika mtoto huyu mdogo, ambaye Maria anamfunika vizuri na upole, ni Mungu wetu aliyejifanya siyo kitu kutokana na upendo wake kwetu. Basi sisi tumpigie magoti kwenye pango alikozaliwa na tumwabudu Mwumbaji wa ulimwengu aliyejifanya kiumbe, Mungu asiyeonekana ameonekana sasa katika umbo la mwili wa mtoto, Bwana mwenyezi wa mbingu na dunia amejionyesha kuwa mdogo na mtoto mchanga mdhaifu mwenye kuhitaji kila kitu, anahitaji hata kupendwa.

Fumbo la kulitafakari na kuliangalia kwa jicho la imani lipo katika kukaona katoto haka kachanga na kujiuliza: Ni kweli katoto haka ni Mungu kweli? Yaani, Mungu akaweza kweli kuuvua ukuu wake mtukufu na wa enzi na kuonekana mbele yetu akiwa mdogo, tena mdogo kabisa kiasi cha kuweza kubebwa mkononi na watu wote, Sababu gani? Jibu lake ndilo ni fumbo linalodai imani ili kulielewa. Wazazi wetu wa kwanza (Adamu na Eva) walidanganywa na nyoka wa kale wakawa na shauku na hamu ya kuwa kama Mungu ili kuwa huru na kuachana kabisa na Mungu.

Wakataka kuwa kama Mungu ili kujilinganisha na kukaa kiti kimoja na Mungu. Wakataka kujitegemea, kuwa huru, kuwa na ukuu, uweza wa kuwa na wa kufanya wanachokitaka wao. Dhambi hiyo ya kutaka kulingana na Mungu ilikuwa kuu sana: yaani kule kutaka kuchukua nafasi ya Mungu na kuwa juu ya Mungu. Huko ni kumfedhi sana Mungu. Ni zaidi ya kumtusi matusi ya nguoni. Ilitosha kabisa Mungu kutumaliza na kutufifisha milele.

Kwa harakaharaka tu Adamu na Eva wakajikuta wamevuliwa nguo wako uchi, maskini, na watu wa kufa. Hata hivyo, hakuna mtu yeyote ambaye angeweza kulirekebisha kosa hili zito na kubwa sana alilokosewa Mungu la kuvuliwa nguo na kiumbe chake. Aidha kutokana na upendo wake mkubwa kwa binadamu, Mungu hakutaka kukipoteza milele kiumbe chake, akajifanya mwenyewe binadamu: Kwa vile kile ambacho hakikuwezekana kwa mtu wa kawaida tu, basi kiwezekane kwa mtu ambaye si mtu tu peke yake bali ni Mungu pia.

Ndiyo maana mtoto aliyelala uchi pale pangoni ni Mungu. Mara nyingi tumesikia tamko hilo, lakini bado hatujagundua kikwazo, na upuuzi wa kibinadamu. Mtoto yule mdogo anayelia, anayecheka, anayenyonya maziwa ya Mama ni Mungu! Inawezekanaje? “Yawezekanaje kuamini kwamba mtoto huyu kuwa ni Mungu… Mungu mkuu, mwenye mamlaka, Mungu wa milele, na kuweza kuishi kama wengine wengi wasiojua hilo, wasiotambua hilo, na wasiosadiki hilo?”.

Kwa hiyo haiwezekani kusadiki kwamba inawezekana kuwa na imani isiyokuwa na vikwazo, mapambano, na isiyotaka kufanya maamuzi. Ndiyo hii, “Inawezekana kabisa kwamba wengi kutosadiki hata kuvutika kuamini eti katoto haka ni Mungu.” Kwa hoja hiyohiyo, ndiyo alitundikwa msalabani. Yaani, Yesu hakusulibishwa kwa sababu alihubiri upendo, la hasha, bali kwa sababu alithibitisha mwenyewe kuwa ni Mungu kama Baba. Hii ndiyo ilikuwa sababu ya kuhukumiwa kifo.

Mtoto huyu atakapokuwa mkubwa, na kuletewa mtu aliyepooza toka juu ya paa lililobomolewa kusudi amponye akasema “Dhambi zako zimeondolewa” hapo wafarisayo wakiwa wamekwazwa wakasema kwa haki “Anakufuru!” Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?” (Lk. 5:21ff). Mtoto huyu atakapokuwa mkubwa atasema pia “Kabla ya Abrahamu mimi nilikuwepo” (Yoh. 8:58) Atakaposhtakiwa kwa kuvunja sabato kwa sababu siku hiyo alikuwa anaponya watu, atasema “Baba yangu anatenda kazi daima, na mimi pia” na hata kutokana na maneno hayo, Wayahudi wakatafuta tena kumwua si kwa sababu alikuwa anavunja sabato, la, bali kwa vile alikuwa anamwita Mungu Baba yake na kufanya mambo sawa na Mungu” (Yoh. 5:16-17).

Katika kiini cha Liturujia la Neno la Mungu, kuna tafakari ya juu kabisa Maingilio ya Injili ya Johani kwamba Neno lililokuwa tangu mwanzo likatwaa mwili na likajenga hema yake kati yetu.

Fumbo mojawapo linalodai imani kulielewa ndilo hili la Neno kuwa mwili (kitu). Kutambua kuwa Mungu aliumba vitu kwa kutamka Neno au jina la kitu hicho- anga, mwanga, dunia nk. Kumbe maneno tutamkayo yanatakiwa yaumbe kitu. Aidha kuelewa pia Neno la Mungu alitwaa mwili akakaa kwetu hapo tungepima zaidi maneno tuongeayo – hasa maneno ya uwongo na ulaghai. Fumbo hili ni kubwa kwamba motto mchanga Yesu ni Neno lililotwaa mwili, ni Mungu kweli.

Walimwua kwa vile alijitangaza kuwa Mungu na hakuwa anatambulika hivyo kwa vile walikuwa na wazo la Mungu lililo tofauti, yaani Mungu mkuu ambaye hakuna nafasi kwa udhaifu, unyonge, manyenyekesho na zaidi Mungu anayekufa tena kufa msalabani! Mungu wa aina hiyo hapendezi kwa binadamu ambao wanampenda Mungu mwenye nguvu, mtukufu, mshindi anayekuokoa tokana na msalaba, mungu asiyekuwa msalabani, Mungu anayekulipa sala zako.

Binadamu wanamtafuta Mungu wa nguvu hivyo, na siyo Mungu wa kubebwa mikononi kama mtoto. Ndugu zangu, Heri kwa Noeli, Nawatakia mtoto Yesu kupokewa ndani yetu kwa mikono miwili, na maisha yetu yakue katika imani yetu na kwa wengine.

2. Hali ya Matumaini:

Katika mtoto huyu mchanga, ambaye Maria anamlaza kwa taratibu na polepole kwenye hori la kulia ng’ombe chakula, tunamtambua kuwa yu Mwalimu, ameketi juu ya kiti chake cha kwanza cha enzi, anaongea kwa nguvu yote mioyoni mwetu. Majivuno ya wazazi wetu wa kwanza yalikuwa ya hali ya juu sana, na hapa unyenyekevu anaoonyesha Mungu hapa wa hali ya juu sana, yaani kujivua kabisa nguo ya utukufu wa kimungu na kuwa mtupu kabisa, na kujionesha kwetu katika hali ya mtoto mdogo na mchanga kabisa.

Kufanya kwake hivyo, si tu anachukua mwili unaokufa ili kuujenga ubinadamu, bali anatuonesha pia njia, namna ya kuweza kuwa Mungu kama Yeye. Maana yake, kama Yeye ni Mungu na ni mtu kweli, hata sisi tulio binadamu tunaweza katika Yeye, na kama Yeye kuwa Mungu yaani “upendo” (IYoh 4:8.16) kwani alimwumba mwanamke na mwanamue “kwa mfano na sura yake” (Mwanzo 1:26) ili waweze kuwa kama Yeye, aliye upendo. Maana yake, hitaji la kuwa kama Mungu, liliwekwa na Mungu mwenyewe ndani ya moyo wa binadamu.

Udanganyifu wa adui shetani halikuwa la kumwelekeza mtu kwenye hitaji hilo la kuwa kama Mungu, bali lilikuwa kuwaongoza binadamu yu Mungu tena Mungu mwenye kupenda mamlaka, mabavu, utawala na siyo Mungu aliye upendo. alimchemsha kwelikweli binadamu kuwa atakuwa kama Mungu lakini bila ya Mungu, maana yake bila ya upendo. Hapa ndipo ilipolala dhambi ya asili inayoendelea kumtafuna binadamu had leo.

Baada ya kupiga magoti mbele ya pango kwa kitoto kichanga, aliye mtoto wa Mungu, na ambaye katika mwili wake mdogo, lakini “anabeba ndani yake utimilifu wa umungu” (Koloseo 2:9) sasa, tutulie mbele yake bila papara, na kumsikiliza anapoongea kwa nguvu moyoni mwetu: ni “Bwana, ni Mwalimu” (Yoh. 13:13) anayetuongelea, ni Mwalimu wa Upendo! Tumsikilize. (Rej. Lk. 9:29) anataka kutueleza nini?

Atazungumzia juu ya utupu wa pango lile, atatutuzungumzia juu ya hori lile alimolazwa, atazungumza juu ya machozi yake ya kwanza aliyotoa na ile tabasamu lake la kwanza, na yote hayo yatatusuta mioyoni mwetu na kutufanya tuonje hali ya kawaida, ya ufukara, ya unyenyekevu, ambayo imeshasahaulika, hali hiyo inukie tena katika maisha yetu. Labda itatufanya tusionje tena utamu wa ulimwengu huu na kuupapalikia. Ulimwengu huu uliojaa kila maraharaha yanayomharibu binadamu na kumdhalilisha.

Alifika ulimwenguni ili kutuvuta tumfuate, kututeka kwa nguvu tamu ya upendo, uzuri na ukweli inayoonekana katika ufukara na unyenyekevu wake. Baadaye atakapokuwa mkubwa mtoto huyu atafundisha: “Njoni kwangu, ninyi nyote mnaoelemewa na mizigo mjifunze kwangu kwani mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo, kwani mzigo wangu ni mtamu na mwepesi (Mt. 11:28-29).

Upole na unyenyekevu, vinatuonesha njia ya ukuu, ya nguvu ya kweli, njia ya utukufu wa kweli. Kutoka pale pangoni, tunasikiliza mahubiri ya kwanza ya Yesu: “Mnataka kuwa wakuu, yaani wakuu hasa? Mnataka kuwa na nguvu na mamlaka, mamlaka hasa? Mnataka kutukuzwa haswa? Basi muwe wanyenyekevu, wapole, muwe wadogo kama nilivyo nilivyowaonyesha mimi leo. Ukweli ni kwamba, mimi nilivyokuwa mkubwa, mkubwa sana… nani mkubwa zaidi ya mimi niliye Mungu? Hakuna. Sasa mimi nimejifanya mdogo tena mdogo kabisa, ili kukufundisha wewe njia ya kuwa mkubwa kama Mimi!

3. Hali ya Upendo:

Tunakitambua kitoto hiki kichanga ambacho kwa furaha yote Maria anakikabidhi kwa wachungaji na Majusi, kisha makundi ya watu wanaopenda ubinadamu huu ulio fukara utakaojitoa wenyewe hadi kufa juu ya msalaba ili kuukomboa ubinadamu. Pale pangoni panatugutia Upendo, tena upendo mkuu wa Mungu kwetu na kwangu. Kwa kweli amezaliwa kwa ajili yangu, kwa ajili yangu Maria anamlaza mtoto pale horini, kwa ajili yangu yuko pale, kwa ajili yangu ananyosha mikono yake, kwa ajili yangu ananifumbulia fumbo la hori lile. Anayesimama pale pangoni kwa imani, budi atakuwa na wazo litakalompeleka Kalvali na kwenye fumbo la upendo lililoisha pale msalabani na alilolitoa kwenye Ekaristi.

Mahali alipozaliwa Yesu panaitwa Betlehemu, jina ambalo kwa kihebrania linamaanisha “nyumba ya mkate” ndiyo nyumba yake ya kwanza, “hori la kulishia wanyama” ndivyo vinavyoimba mioyoni mwetu kuwa Yeye ni Mkate ulioshuka toka mbinguni (Yoh. 6:51) atakayetakiwa atolewe kwa ajili ya wokovu wetu. Hori lile alimolazwa ndiyo tabernakulo ya kwanza, ambamo “Mwanakondoo” (Yoh. 1:29) anapotolewa sadaka mara ya kwanza kwa ajili yetu, anajitoa kwetu ili aliwe: “Asiyekula mwili wangu na asiyekunywa damu yangu hana uzima… Anayenila mimi, ataishi kwa ajili yangu” (Yoh. 6:53.57).

Kila Noeli Mama Bikira, kwa njia ya kanisa, tunaalikwa kumshika mtoto mikononi kama wachungaji, kama Majusi, kama kila mtu anayeingia mle pangoni. Yeye mtoto mchanga ananyosha mikono yake midogo kwa wote ili ashikweshikwe na kubebwa na wote: Hilo ndilo fumbo la Noeli! Vingine hiyo siyo Noeli endapo humshiki mtoto Yesu mkononi, kama humbembelezi, humbusu. Kutokana na hilo, Yesu amezaliwa kwa ajili yako, kwa ajili yangu: “Tumepewa mtoto” (cf Is. 9:5), kwa kweli ni wetu, kweli ni wangu, ni wako!Tukifanya hivyo, tukimshika mtoto mikononi mwetu basi maisha yetu yatabadilika.

Kutokana na hiyo, Yeye anataka kubebwa mkononi! Kwa sababu baada ya kumshika yeye, tutaweza kuendelea kutumia mikono yetu ileile iliyomshika ili kujilundikia mali, kujivua, na kufurahia ukuu? Utawezaje kuangalia macho yake machanga ya kawaida na kuendelea bado kuzama katika uovu, wivu na kila ubaya? Utawezaje kumbeba mtoto kifuani na kuendelea bado kujichafua moyo wako na madhambi? Huko ni kujipinga kabisa. Kutokana na hiyo, kila noeli Bikira Mtakatifu anatukabidhi mtoto wake tumshike mikono na kumbeba kifuani petu!

Tafakari hii imeandaliwa na kuletwa kwako na Padre Alcuin Nyirenda, OSB.









All the contents on this site are copyrighted ©.