Waamini walei Injilisheni kwa kuyatakatifuza malimwengu!
Askofu Beatus Kinyaiya wa Jimbo Katoliki Mbulu, Tanzania, ni kati ya Mababa waliohudhuria
Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya iliyohitimishwa hivi karibuni hapa mjini
Vatican.
Katika mahojiano
maalum na Radio Vatican anasema kwamba, Viongozi wa Kanisa wanaendelea kuhimizwa kutoa
majiundo makini kwa waamini walei ili waweze kushiriki kikamilifu katika maisha na
utume wa Kanisa.
Wakati umefika kwa waamini Barani Afrika kujivunia dhamana
waliyojitwalia kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, kwa kutoka kimaso maso kwenda sehemu
mbali mbali za maeneo yao kumtangaza Kristo, lakini zaidi kumshuhudia kwa njia ya
maisha yao adili na manyofu. Vyama vya kitume visaidie harakati za Kanisa katika azma
ya Uinjilishaji Mpya, kwa kuwashirikisha waamini wengine karama na malengo ya vyama
hivi.