2012-12-22 12:55:16

Ushirikiano kati ya Kanisa na Serikali unapania kuboresha huduma ya afya Mkoani Mbeya


Mheshimiwa Padre Renatus Mwakanyamale, Katibu wa Afya, Jimbo Katoliki Mbeya ameishukuru Wizara ya Afya kwa kuwa na ushirikiano mzuri na Kanisa kupitia huduma ya afya inayotolewa na Kanisa. Licha ya kuwa na uhaba wa watumishi na vifaa lakini bado juhudi za Serikali katika kuhakikisha tatizo hilo linapunguwa ama kumalizika zinaendelea na hivyo kutia moyo wa kuendelea kutoa huduma hiyo.

Padre Mwakanyamale ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Mbalizi amesema, katika miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na ushirikiano na mahusiano mazuri baina ya Halmashauri za Wilaya ya Rungwe, Chunya na Mbozi ambako Jimbo Katoliki la Mbeya linatoa huduma zake za afya kwa kuwapelekea watumishi na vifaa tiba hali inayodhihirisha kutekeleza kwa vitendo mkataba wa makubaliano ya utoaji wa huduma za afya kwa jamii (Service Agreement).

Aidha Padre Mwakanyamale alisema tatizo ambalo limebakia ni ucheleweshwaji wa fedha ya ruzuku kwenda katika maeneo ambako huduma hizo zinatolewa na hivyo kuleta usumbufu mkubwa lakini ana imani Serikali ni sikivu italifanyia kazi kwa kulitafutia ufumbuzi wa kudumu.

Padre Mwakanyamale anabainisha kwamba, Jimbo Katoliki la Mbeya lina Hospitali mbili teule za Wilaya ambazo ni Igogwe iliyopo Wilayani Rungwe na Mwambani iliyopo Wilayani Chunya, vituo vya afya viwili ambavyo ni Mkulwe na Kisa pamoja na Zahanati 22 zikiwemo za Iyunga kwa Mbeya mjini na Lupa, Totowe na Mbuyuni, Wilayani Chunya ambazo zipo katika mchakato wa kupandishwa hadhi ili kuwa ni Vituo vya afya.









All the contents on this site are copyrighted ©.