2012-12-21 15:58:27

Wafugaji na wakulima heshimianeni ili kulinda na kukuza amani, upendo na mshikamano katika Jamii


Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameahidi kuchangia sh. milioni 20 za kuanzia ujenzi wa kituo cha afya katika kata ya Mwamapuli ili kiweze kusaidia kata za jirani za Mbede na Majimoto.

Alitoa ahadi hiyo Alhamisi, Desemba 20, 2012 wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Mwamapuli kwenye mradi wa mashine ya kukoboa mpunga akiwa katika siku ya nane ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.

“Hapa Mwamapuli hatuhitaji tena kuzungumzia habari ya zahanati sababu mmezungukwa na vijiji vingi na kata nyingi. Mnahitaji kituo cha afya ili kata za jirani za Mbede na Majimoto ziweze kunufaika,” alisema.

Waziri Mkuu ambaye ni mbunge wa jimbo la Katavi aliwaambia wakazi hao kwamba wakimaliza kazi ya kuvuna, waweke mpango mahsusi wa kuchangia matofali kwa kila kaya, na kila kijiji ili kusaidia ujenzi wa kituo hicho.

Aliwasihi watendaji na wenyeviti wa vijiji wasiwabugudhi wananchi kuhusu michango hiyo hadi watakapomaliza msimu wa kilimo. “Tuwaache wamalize kuvuna ndipo wachangie, tunataka kituo hiki kiwe kimefunguliwa ifikapo mwaka 2015,” alisema huku akishangiliwa.

Pia aliwataka wafugaji na wakulima wakae kwa kuheshimiana. “Wafugaji lazima tuendelee kuheshimu wakulima, tusipeleke mifugo kwenye mashamba yao. Kuheshimiana ndiyo kutatuondolea balaa la kupigana,” alisisitiza.

Wakati huo huo Waziri mkuu ameahidi kutoa sh. milioni tano kwa wafuga nyuki 10 wa kijiji cha Mbede katika kata ya Mbede ili ziwasadie kutengeneza mizinga ya kisasa.

Alitoa ahadi hiyo Alhamisi, Desemba 20, 2012 wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Mbede kwenye uwanja wa shule ya msingi Mbede akiwa katika siku ya nane ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.

Waziri Mkuu aliuliza kwenye mkutano huo wa hadhara wangapi wana mizinga ya nyuki wakajitokeza watu hao 10. Alipowahoji kila mmoja, alibaini kuwa jumla yao wote wana mizinga 115 na zaidi ya mizinga 60 ina nyuki lakini akabaini kuwa wote wanatumia mizinga ya asili ya kutundika juu ya miti.

“Nataka muanze kufuga kisasa… Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mpanda itabidi usimamie zoezi la kutengeneza mizinga hii ili kikundi hiki kiwe kichocheo cha mabadiliko kwa wengine katika kata hii,” alisema.

“Achaneni na hiyo mizinga ya asili kwa sababu uzalishaji wake ni mdogo, na kazi ya kuparamia ina adha zake… kwenye mizinga ya kisasa unaweza kucheki nyuki kama wameingia kwenye mzinga kadri unavyotaka,” alisema.

Waziri Mkuu ambaye ni mbunge wa jimbo la Katavi aliwaambia wakazi hao kwamba nyuki wanaweza kufugwa kama ilivyo kwa mifugo mingine. “Wanataka kuwekewa maji, mabanda yao yanataka kusafishwa kila mara, na hii itakuwa rahisi kama tu mtatumia mizinga ya kisasa,” alisisitiza.

Waziri mkuu amewataka wakulima wa kata ya Mwamapuli wakubaliane kula njama na wakatae kuuza mpunga kutoka bonde la Rukwa ili wanunuzi wote wanunue mchele badala ya mpunga.

Alitoa rai hiyo Alhamisi, Desemba 20, 2012 wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Mwamapuli kwenye mradi wa mashine ya kukoboa mpunga akiwa katika siku ya nane ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.

Alisema kuuza mchele kutaongeza thamani ya zao hilo na hivyo kufanya bei iwe juu. “Itabidi diwani na viongozi wengine wakae na wananchi na kupanga bei ya kuuza mchele wao ili kuwa na sauti ya pamoja,” alisema.

Alisema mashine hiyo ya kukoboa ina uwezo wa kukoboa magunia 400 kwa siku kwa hiyo wana uhakika wa kusindika kile wanachokizalisha.

Waziri Mkuu ambaye ni mbunge wa jimbo la Katavi aliwaambia wakazi hao kwamba wafuate kanuni bora za kilimo na kuwasisitiza kulima mpunga kwa kufuata mistari ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo kwa kila ekari.









All the contents on this site are copyrighted ©.