Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Nne ya Kipindi cha Majilio
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, kipindi tafakari masomo ya Dominika, tunaendelea
na safari yetu tukiwa sasa Dominika ya 4 ya Kipindi cha Majilio Mwaka C wa Kanisa.
Mpendwa
katika Dominika hii tunaongozwa na Nabii Mika, mwandishi wa barua kwa Waebrania na
kama kawaida mwinjili Luka. Nabii Mika anatangaza wokovu kwa watu waliowaaminifu kwa
Mungu. Anaishi karne ya nane ambapo kuna unyonyaji dhidi ya maskini unaofanywa na
matajiri. Akiwa upande wa maskini anasema hawa wanyonyaji wataadhibiwa na Mungu, kumbe
anatangaza tumaini kwa waliomaskini.
Nabii Mika anatangaza kuzaliwa kwa Masiha
katika mji wa Betlehemu - Efrata, mji ambao ni mdogo bila thamani mbele ya watu lakini
wenye thamani mbele ya Mungu, maana atazaliwa huko mfalme wa amani na mtawala wa Israeli
mpaka miisho ya dunia. Efrata ni famila ndogo ya kabila la Yuda ambapo kwanza anazaliwa
Daudi na Kisha Mfalme Mkuu yaani Yesu Kristo Masiha. Huyu atakuwa Mchungaji wa kondoo
na mchungaji mwema. (Yn. 10) Mfalme huyu ni Mfalme wa amani kwa sababu ni mwenye upendo
kwa Mungu na kwa jirani.
Mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu, mwandishi wa
barua kwa Waebrania anawaandikia watu walioongekea ukristu na kwa namna hiyo anataka
kuwaimarisha katika imani yao. Anawaambia kuwa Kristo ni yule aliyetabiliwa katika
Agano la kale, kwa namna hiyo basi anakamilisha uaguzi huo anaposhuka kwetu. Anakazia
mafundisho yake akiwaambia Kristo anatolea sadaka moja tu ya Kalvari kwa milele na
inatosha kwa ondoleo la dhambi zetu zote. Kristo anamtii Mungu na hivi anachukua nafasi
ya dini ya zamani na yeye anakuwa mlango wa utakatifu na Imani yetu ya Kikristo.
Kwa
utii anakuwa kipatanisho chetu kati yetu na Mungu Baba na kwa namna hiyo anaondoa
matambiko na sadaka za kale na tunaanza maisha mapya. Tukifuatilia vema mtililiko
wa tafakari ya mwandishi tunaona pia sisi wenyewe baada ya ubatizo hatuko katika maisha
ya zamani bali maisha mapya, maisha si kivuli ba halisia katika Masiha. Kwa njia hiyo,
tunajiunga na utakatifu wa Yesu Kristo na hivi kama yeye alivyoyafanya mapenzi ya
Baba yake nasi twaweza kutimiza mapenzi ya Mungu. Baada ya kazi hiyo takatifu basi
matunda ni uzima wa milele na ni matokeo ya sadaka moja ya Bwana.
Katika somo
la Injili tunapata kuingizwa katika furaha ya Krismasi, tunaalikwa kuweka nguvu zetu
pamoja katika Kristu kwa kielelezo cha wanawake wawili, Maria na Elizabeti, ambao
ni wazazi wa Yesu Kristo na Yohane mbatizaji. Mwinjili anatufundisha kuwa Elizabeti
anashiriki furaha ya Maria na anatamka waziwazi kuwa Maria ni mbarikiwa! Kukutana
kwa mama hawa 2 ni kukutana kwa Masiha na Yohane Mbatizaji.
Mpendwa, tunapotafakari
kukutana kwa Mama hawa lazima tujiulize kwa nini Maria aende kumtembelea Elizabeti?
Kwa maana kwanza kati ya kijiji cha Maria na Elizabeti kuna mwendo wa kutosha na isitoshe
ni milimamilima! Lazima Maria asukumwe na jambo la maana, liletalo furaha katika maisha
yake. Kwa hakika anataka kushiriki furaha ya Elizabeti aliyekuwa bila mtoto kwa muda
wa kutosha sasa atapata mtoto, Mungu anatenda maajabu, kwa maana hakuna aliyetegemea
tena kuwa Elizabeti atapata mimba!
Mpendwa, nasi tunafuata nini kanisani, katika
jumuiya? Tunaifuata furaha ya Bwana, tunavutwa na upendo wa Mungu asemaye, njooni
kwangu ninyi nyote msumbukao na kulemewa na mizigo! Tendo la safari ya Maria si la
kimwili tu bali lagusa roho, ni kwenda kwa Mungu. Kumbe, nasi tunaalikwa kwenda kukutana
na wale waliotembelewa na Mungu ndio majirani zetu, wanajumuiya wenzetu na kanisa
kwa ujumla. Maria anapofika kwa Elizabeti anashiriki furaha ya Elizabeti na kisha
Elizabeti anashiriki furaha ya Maria na mtoto Yesu. Namna hii yapaswa kuwa maisha
ya jumuiya kila mmoja lazima agawe vipaji vyake kwa wengine. Mtakatifu Ursula anasema
kila mtawa awe ni hostia safi kwa mwenzake.
Mpendwa, katika Maadhimisho ya
mwaka huu wa Imani ambao Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita ameuzindua rasmi
hapo tarehe 11Oktoba 2012, tunapaswa kuwa waamini ambao si tu wa kujua yaliyomo katika
Imani bali kuyaishi ili yaweze kuzaa furaha ambayo ni kwa ajili ya wengine. Imani
hukolea mara mwaliko wa kufungua mioyo yetu, kiti kitakatifu cha mwanadamu unapokamilika
na kuwekwa katika mtiririko wa maisha yak ila siku.
Maria yu na Bwana na Elizabeti
anapokea furaha ya Bwana kwa njia ya Maria, kumbe hawa wote wa wawili wanayoimani
na wa,maefungua mioyo yao kupokea furaha kuu. Ni wajibu wako ndugu mpendwa kufungua
moyo wako ili kuishi zawadi ya imani iliyo ya kweli.
Nikutakie sherehe njema
ya Noeli, Mtoto Emanueli anayekuja kwetu azaliwe katika moyo wako uliomwongokea yeye
furaha ya milele. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd.
Richard Tiganya, C.PP.S.