Salam za Noeli na Matashi mema kutoka kwa Papa Benedikto XVI kwa wasaidizi wake wa
Karibu
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Ijumaa, tarehe 21 Desemba 2012 aliungana
na wasaidizi wake wa karibu kama Familia, kutakiana matashi mema katika maadhimisho
ya Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2012, wakiungana pamoja kama Familia kumwabudu Mtoto
Yesu ambaye ni Mungu aliyejifanya mtu ili aweze kuwa karibu zaidi na mwanadamu. Anawashukuru
wote waliomwezesha kutekeleza utume wake sehemu mbali mbali za dunia.
Mwaka
2012 unaoyoyoma kwa kasi umesheheni maswali mazito, changamoto na matumaini katika
maisha ya Kanisa na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Amezungumzia baadhi
ya matukio haya kuwa ni hija yake ya kichungaji nchini Mexico na Cuba; mahali ambako
ameshuhudia waamini wakiwa wamesheheni furaha inayobubujika kutoka katika Imani; vijana
waliokuwa wamepiga magoti kandoni mwa barabara wakipokea baraka kutoka kwa Khalifa
wa Mtakatifu Petro.
Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu karibu na Sanamu
ya Yesu Kristo Mfalme, yalidhihirisha kwa namna ya pekee Ufalme wa Kristo unaojikita
katika: amani, haki na ukweli; licha ya hali mbaya ya kiuchumi wanayokabiliana nayo
wananchi wameonesha ari ya kutaka kujisafisha kutoka katika undani wa mioyo yao wakisukumwa
na nguvu ya imani pamoja na kukutana na Yesu Kristo.
Ibada ya Misa Takatifu
nchini Cuba ilionesha uwepo wa Mungu ambaye kwa miaka mingi hakupewa nafasi nchini
humo, kwa hakika watu wanapaswa kufanya rejea kwenye tunu msingi ambazo zimejionesha
kwa namna ya pekee katika maisha ya mwanadamu kwa kukutana na Mungu wa Yesu Kristo.
Baba Mtakatifu amegusia pia Maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa, Hija
yake ya Kichungaji nchini Lebanon alikokwenda ili kuzindua matunda ya Sinodi ya Maaskofu
Katoliki Mashariki ya Kati, Waraka unaopaswa kuwa ni dira na mwongozo wa maisha na
utume wa Kanisa Mashariki ya Kati, katika mchakato wa ujenzi wa msingi ya umoja na
amani. Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya, Mwaka wa Imani
sanjari na Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ni kati ya matukio
muhimu sana yaliyojiri katika mwaka huu.
Umekuwa ni muda wa kutafakari kwa
kina kuhusu familia: kinzani, vikwazo na umuhimu wake katika kurithisha tunu msingi
za maisha yamwanadamu kiroho na kimwili; ni shule ya umoja na mshikamano wa dhati,
kwa kuishi na kusumbukiana kwa pamoja; kwa hakika familia inagusa undani wa mtu. Kinzani
zinazojitokeza ni ile hali ya uhusiano tenge kati ya watu; uhusiano ambao hauwajibishi
na unaokwenda kinyume cha utu, heshima, uhuru na utimilifu wa binadamu. Watu wanataka
kuwa na uhuru usiokuwa na mipaka bila kufungwa na kifungo cha upendo hadi mauti; watu
wanataka kuukimbia ukweli na kujifunga katika ubinafsi wao.
Baba Mtakatifu
anakumbusha kwamba, mtu kwa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya familia na wengine,
hapo anaweza kupata utimilifu wa maisha, vinginevyo, watoto wanaweza kujikuta kwamba
wanakabiliwa na uwepo wa wazazi ambao wana mwelekeo tofauti kabisa na mapokeo; yaani
wazazi wenye jinsia moja! Hizi ni dalili za kumong'onyoka kwa tunu msingi za kifamilia
na kuporomoka kwa uhuru wa binadamu na asili yake kama mwanaume na mwanamke.
Dhana
ya jinsia imepewa nafasi maalum katika Jamii inayojipambanua yenyewe badala ya Jamii
kuipambanua dhana hii. Ni dhana inayopinga asili ya mtu kadiri ya mpango wa Mungu
katika kazi ya uumbaji. Jamii inajitwalia madaraka ya uumbaji wa mwanaume na mwanamke;
mwanadamu anakabiliwa na hali ya kuishi katika utupu, kinyume kabisa na asili pamoja
na kazi ya kuendeleza uumbaji. Ni uhuru usiokuwa na mipaka kiasi hata cha kutotambua
uwepo wa Mungu. Kinzani dhidi ya familia ni mchezo hatari unaomhusisha mtu na utu
wake, kwani yeyote yule anayepigania uwepo wa Mungu anampigania pia mwanadamu.
Uinjilishaji
Mpya ni juhudi za Kanisa katika kukuza na kudumisha majadiliano pamoja na kuendelea
kutangaza Injili ya Kristo; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima
ya mwanadamu; majadiliano na Serikali pamoja na majadiliano na Jamii mintarafu mwanga
wa Imani unaoonesha ufunuo wa Mungu kwa mwanadamu katika historia yake. Ulimwengu
bila kumbu kumbu za kihistoria unapoteza utambulisho wake. Kanisa linapojadiliana
na Serikali halina majibu ya mkato, bali linapania kusimama kidete kulinda na kutetea
tunu msingi za maisha ya kiroho na kimwili; mambo yanayoweza pia kumwilishwa katika
shughuli za kisiasa.
Majadiliano ya kidini na kiekumene ni kati ya mambo yanayoendelea
kupewa kipaumbele na Mama Kanisa katika maisha na utume wake; majadiliano yanayosimikwa
katika uhalisia wa maisha na mshikamano wa dhati. Ni mahali pa kushirikishana Imani
katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, Biblia pamoja na kuangalia matatizo na changamoto
zinazomkabili mwanadamu katika ulimwengu mamboleo. Jamii, Serikali na Kanisa waweze
kuwajibika kwa pamoja katika kulinda na kudumisha: ukweli, haki, amani, misingi ya
maadili na utu wema. Ni mwaliko wa kujenga utamaduni wa kusikilizana, kusaidiana ili
kujisafisha na hatimaye, kutajirishana, kwa kutambua na kuheshimu tofauti zao za msingi
zinazojikita katika ukweli na amani.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, kuna sheria
mbili zinazoratibu majadiliano ya kidini, yaani majadiliano yasilenge kumwongoa mtu
bali kufahamiana; hapa Kanisa linatofautisha kati ya Uinjilishaji na utume wake. Pili
ni kuimarisha ukweli uliofikiwa na pande hizi mbili katika utambulisho na makubaliano
yake, ili kuweza kufikia umoja katika ukweli. Wakristo wanatambua kwamba, Kristo ndiye
Ukweli wanaoutafuta na kuukumbatia kwa dhati, kiasi cha kuambatana na kusonga mbele
na Kristo kwa ujasiri mkuu kwani Yeye ni mwanga wa ukweli.
Baba Mtakatifu anabainisha
kwamba, Uinjilishaji Mpya ni mchakato wa kumtambulisha Kristo kama Mwanakondoo wa
Mungu anayeondoa dhambi za dunia, Masiha na Mkombozi wa Ulimwengu. Ni mwaliko wa kumfuasa
Kristo ili kumfahamu zaidi ili aweze kuzima kiu na udadisi wa wafuasi wake, kwa kuwafungua
macho ili kuona matendo makuu ya Mungu.
Ili Neno la Mungu liweze kuota mizizi
yake kuna haja kwa mwamini kuonesha moyo wa unyenyekevu, kwa kutamani kumfahamu zaidi
Kristo na hatimaye kukutana naye ndani ya Kanisa, sehemu ya Fumbo la Mwili wake Mtakatifu;
tayari kujenga na kuimarisha umoja katika maisha wakiwa macho zaidi. Licha ya umaskini
na mapungufu yake, Kanisa anasema Baba Mtakatifu halina budi kuonesha uhai, ili kuzima
kiu na shauku ya mwanadamu inayomtafuta Yesu, Mungu kweli na Mtu kweli.
Baba
Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa wasaidizi wake wa karibu kwa kuwatakia kheri
na baraka kwa Siku kuu ya Noeli na Mwaka Mpya 2013.