2012-12-21 10:33:30

Noeli kiwe ni kipindi cha kukuza na kuimarisha udugu, umoja, furaha, amani, matumaini, upendo na mshikamano!


Baraza la Maaskofu Katoliki Uruguay katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha, hasa kwa wanyonge na watu wasiokuwa na sauti. Inasikitisha kuona kwamba, kadiri siku zinavyozidi kusonga mbele, zawadi ya uhai inaendelea kuwa mashakani, kiasi kwamba, kuna baadhi ya watu hawaoni tena thamani ya maisha, kiasi cha kuichezea wanavyotaka!

Mama Kanisa wakati huu wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kujenga na kuimarisha umoja, udugu, mshikamano wa upendo na ukarimu, kama njia muafaka ya kumkaribisha tena Mtoto Yesu anayezaliwa katika maisha na mioyo ya watu.

Maaskofu Katoliki Uruguay wanasema, furaha ya Mama Kanisa kwa wakati huu inabubujika kutokana na kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa Dunia; anayekuja kumshirikisha mwanadamu furaha, upendo na huruma ya Mwenyezi Mungu.

Ni mwaliko wa kutoka katika matendo ya giza na mauti na kuanza safari inayomwelekeza mwamini katika furaha inayothamini na kuendeleza zawadi ya maisha, dhidi ya tamaduni za kifo zinazoendelea kuibuka kwa nguvu ya ajabu. Watu wajifunze kuthamini maisha ya binadamu katika hatua mbali mbali za makuzi yake; wakuze fadhila ya matumaini ambayo kamwe hayawezi kudanganya na daima wajitahidi kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano kati ya watu.

Hii ndiyo njia bora zaidi ya kuweza kuadhimisha Siku kuu ya Noeli kwa kukataa kabisa kishawishi cha utengano na uvunjaji wa sheria za nchi. Ni furaha inayojikita katika utambuzi wa uwepo wa Mungu kati ya watu wake na kwa njia hii, Kanisa linaweza kuwafikia watu mbali mbali katika hija ya maisha yao hapa duniani, ili kuwaonjesha ile furaha ya kuzaliwa kwa Mtoto Yesu, Mfalme wa Amani.

Ni matumaini ya Maaskofu Katoliki Uruguay kwamba, Siku kuu ya Noeli itawawezesha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kugundua na kukuza ndani mwao ari na moyo wa udugu, furaha, ukarimu, matumaini, amani na maendeleo ya kweli, yanayojali utu na heshima ya kila mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.