2012-12-21 07:28:30

Mwaka wa Imani uwe ni kichocheo cha kuifahamu, kuiimarisha na kuimwilisha imani katika matendo ya huruma na upendo!


Askofu Alfred Agyenta wa Jimbo katoliki Navrongo, Ghana, katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, anawaalika Watu wa Familia ya Mungu Jimboni mwake, kutumia vyema maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ili kuifahamu, kuiimarisha na kuimwilisha Imani yao kwa njia ya vitendo; daima wakijitahidi kumwongokea Mwenyezi Mungu, kwa kukumbatia fadhila za maisha adili. RealAudioMP3

Uwe ni Mwaka wa Neema na Baraka. Waamini washirikiane kwa karibu zaidi na viongozi wao wa maisha ya kiroho, ili kufanikisha mikakati na malengo ya Mwaka wa Imani pamoja na kufanya tafakari ya kina kuhusu Fumbo la Msalaba ambao utatembezwa Jimboni humo wakati wote wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Waamini watambue na kuthamini Msalaba unaonesha upendo wa hali ya juu kabisa ulioneshwa na Kristo kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.

Mwaka wa Imani iwe ni fursa ya kufanya tafakari ya kina kuhusu tunu msingi za maisha bora ya Familia kwa kujitahidi kuiga Mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, iliyoonesha imani na matumaini makubwa kwa Mwenyezi Mungu; ikawa ni kielelezo thabiti cha Injili ya Upendo kwa Mungu na Jirani; Ibada na bidii ya kazi. Familia ya Kikristo ni Kanisa dogo la nyumbani, ni shule ya utakatifu, haki, amani, upendo, mshikamano na msamaha wa kweli. Kwa maelezo haya, Familia inakuwa ni Hekalu, mahali panapoonesha na kudhihirisha uwepo wa Mungu.

Familia ya kweli na inayodumu, ni ile inayosali kwa pamoja. Mwaka wa Imani uwe ni chachu kwa Wanafamilia kushiriki kwa pamoja katika Maadhimisho mbali mbali ya Sakramenti za Kanisa, lakini zaidi katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa; bila kusahau Sakramenti ya Upatanisho, inayomwonjesha mwamini huruma na upendo wa Mungu; tayari pia kumwilisha tunu hizi katika uhalisia wa maisha, kwani hii ni Imani katika matendo.

Waamini wajifunze kusali, kusoma na kulitafakari Neno la Mungu kwa pamoja. Wazazi watambue na kuthamini wajibu wa kuwafunza na kurithisha Imani pamoja na tunu msingi za kimaadili kwa watoto wao. Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki iwasaidie wazazi kujiandaa vyema kuwashirikisha na kuwarithisha watoto Imani wanayoungama, wanayoiadhimisha, wanayoimwilisha na kuisali, ili iweze kuwa ni sehemu ya vinasaba vya maisha ya watoto wao tangu mwanzo, kwani mtoto umleavyo ndivyo akuavyo!

Waamini wanakumbushwa kwamba, Parokia ni Jumuiya ya Waamini inayoonesha uhai, maisha na utume wa Kanisa mahalia. Hapa waamini wanapata fursa ya kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa; wanajenga na kuimarisha uhusiano wao na Mwenyezi Mungu pamoja na jirani zao. Ni mwaliko kwa waamini kujenga na kudumisha utamaduni wa Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu.

Wahamasike kufanya hija za maisha ya kiroho ili kujipatia rehema kamili zinazotolewa na Mama Kanisa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kwa kutekeleza masharti yaliyowekwa, yaani: kupokea Sakramenti ya Upatanisho, Ekaristi Takatifu na Kusali kwa nia ya Baba Mtakatifu. Mwaka wa Imani, ulete hamasa ya kutolea ushuhuda makini wa Imani katika matendo.

Waamini wajifunze kwa moyo sehemu muhimu za Ibada ya Misa Takatifu ambazo mara nyingi zinaimbwa: kwa mfano: Utukufu, Kanuni ya Imani na Sala ya Baba Yetu ambayo kimsingi ni muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Yesu. Hii ni hazina ya Imani.








All the contents on this site are copyrighted ©.