Papa ajibu Ombi la Gazeti la TIMES: asema Wakristo na Watu wenye mapenzi mema wajitahidi
kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya mshikamano wa upendo!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amekubali na kujibu ombi la Gazeti la TIMES
kuwamegea wasomaji wa Gazeti hili mawazo yake mintarafu kitabu chake kuhusu Simulizi
za Utoto wa Yesu, kilichochapishwa hivi karibuni, kama sehemu ya maadhimisho ya Siku
kuu ya Noeli kwa Mwaka 2012.
Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu amekwisha
wahi kupokea maombi kama haya kutoka kwa Shirika la Utangazaji Uingereza, yaani BBC
baada ya kuwa amehitimisha hija ya kichungaji nchini Uingereza. Ombi kama hili pia
lilikwisha kutolewa na Kituo cha Televisheni cha Taifa, Italia, alipokuwa anajibu
maswali katika Maadhimisho ya Ijumaa kuu.
Baba Mtakatifu anapenda kutumia
fursa hii, kushirikisha mawazo yake wakati huu Mama Kanisa anapojiandaa kuadhimisha
Fumbo la Umwilisho, kwa kuhakikisha kwamba, waamini wanajihusisha na maisha duniani
kwa kumpatia Mungu kile kilicho cha Mungu na Kaisari, yale yaliyo ya Kaisari bila
kumwingiza Yesu katika majaribu kama walivyotaka kufanya Mafarisayo. Waamini wasichanganye
mambo ya kidini na kidunia kwa nia ya kuchuma mali na kujipatia utajiri. Yesu alitumia
fursa ile kuweka bayana kuhusu utawala wake kwamba, haukuwa ni wa dunia hii.
Baba
Mtakatifu anasema kwamba, Simulizi za Maisha ya Utoto wa Yesu katika Agano Jipya zinaonesha
kwamba, alizaliwa wakati wazazi wake wakishiriki katika zoezi la kuhesabu watu, wakati
wa utawala wa Kaisari Augusto. Mtoto Yesu alizaliwa kwenye mazingira duni kabisa,
lakini, huyu ndiye anayeleta amani duniani inayopita nyakati na mahali. Ni Mfalme
anayeshinda dhambi na mauti kwa njia ya mateso na kifo chake.
Kuzaliwa kwa
Yesu ni changamoto kwa Jumuiya ya Kimataifa kulinda na kuthamini zawadi ya maisha;
ni fursa ya kuchunguza dhamiri hasa zaidi kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa,
ambao umesababisha madhara makubwa katika maisha ya watu na kile ambacho watu wanaweza
kujifunza kutokana na unyenyekevu, umaskini na ukawaida wake. Noeli kiwe ni kipindi
cha kusoma na kufanya tafakari ya kina kuhusu Maandiko Matakatifu, ili kumtambua Kristo
ambaye ni Mungu kweli na Mtu kweli.
Wakristo popote pale walipo, wajitahidi
kuyatakatifuza malimwengu, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi:
kwa kupambana na umaskini na kuendelea kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima
ya kila mwanadamu; watumie vyema rasilimali ya dunia na wawe ni watunzaji bora wa
mazingira, wakionesha mshikamano wa upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa Jamii, ili kujipatia utimilifu wa maisha.
Kila mtu anachangamotishwa kuwa
ni mjenzi wa msingi wa haki na amani. Wakristo washirikiane na waamini wa madhehebu
na dini mbali mbali katika kutekeleza wajibu na dhamana yao kwa Mungu na katika dunia
hii. Wajitahidi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mungu na kamwe wasiabudu miungu wa
uongo.
Kuzaliwa kwa Yesu Kristo ni kielelezo cha mwanzo mpya dhidi ya utawala
wa Mfalme Kaisari Augusto ambao hakuwa na mpinzani kwa karne nyingi. Yesu ni Mfalme
wa Amani na Matumaini kwa wote wanaoishi katika wasi wasi na hali ngumu ya maisha.
Kutoka katika Pango alimolazwa, anawaalika watu wote wenye mapenzi mema kushikamana
ili kujenga dunia iwe ni mahali pazuri pa kuishi.