2012-12-20 14:18:43

Muasisi mkuu wa maisha, furaha, upendo, amani ni Mungu ambaye amejifanya mtoto katika Nafsi ya Yesu Kristo!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Alhamisi tarehe 20 Desemba, 2012 amewashukuru wajumbe wa Chama cha Vijana Wakatoliki Italia waliofika kumtakia matashi mema kwa Siku kuu ya Noeli kwa mwaka 2012. Kauli mbiu ya majiundo endelevu ya vijana hawa inawaalika kwa kusaidiana na walezi wao kumtafuta "muasisi", ili hatimaye, waweze pia kusaidiana na vijana wengine.

Baba Mtakatifu anafahamu kwamba, vijana hao wanamtafuta muasisi wa maisha atakayewasaidia kuishi vyema, wakiwa wameridhika wao pamoja na wenzi wao! Huyu ni Mwenyezi Mungu ambaye amewafunulia uso wake; amewaumba kwa sura na mfano wake, lakini zaidi, amewakirimia Mwanaye wa Pekee, Yesu Kristo, aliyejinyenyekesha na kuwa kama mtoto atakayezaliwa tena katika kipindi cha siku chache kuanzia sasa. Ni mtoto aliyekuwa na kukomaa kama vijana hao, akafanya hija ya maisha hapa duniani ili kutangaza upendo wa Mungu unaowawezesha watu kuwa wema na wenye furaha na wakarimu.

Mungu ndiye muasisi wa chemchemi ya furaha ambayo haipatikani kwenye michezo, kati ya marafiki na wazazi wanaowapenda fika na kuwamegea furaha, lakini Yesu ndiye Rafiki yao mkubwa anayejaza mioyo yao kwa furaha ya kweli na endelevu katika maisha yao yote; changamoto kwa vijana kujitaabisha kumjifunza, kumfahamu na kujadiliana naye ili kuweza kuridhika katika maisha na kwa njia hii, wataweza pia kushinda machungu madogo madogo ambayo wakati mwingine yanakuwemo ndani ya mioyo.

Vijana kama wanamtafuta muasisi wa maisha, kamwe hawawezi kujifungia katika ubinafsi wao, bali wanapaswa kujibidisha kutafuta mema na kujisikia kwamba, kuna mtu anayewatakia mema katika hija ya maisha yao, jambo msingi linalomwezesha mwanadamu kuishi vyema; lakini pia vijana hawa wanapaswa kufahamu namna ya kupenda wengine, kuthamini zawadi ya maisha kwa wote lakini zaidi kwa wale wanaokumbana na hali ngumu ya maisha. Yesu kwa njia ya mfano wa maisha yake, amewawezesha waamini kufahamu upendo wa Mungu ambao hauna mipaka na kwamba, anataka kila mtu aweze kuishi kwa furaha.

Baba Mtakatifu anawashukuru Vijana Wakatoliki Italia kwa kuchangia gharama za kuendesha mradi unaopania kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu, nchini Misri. Kwa hakika, vijana hawa wanatafuta chemchemi ya amani katika maisha yao, ambayo kamwe haiwezi kupatikana kwa juhudi za mtu mmoja, lakini wafahamu kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye anayeweza kuwapatia amani ya kweli na yenye kudumu.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anahitimisha shukrani zake kwa vijana hawa kwa kuwataka kutoa nafasi katika maisha yao kwa ajili ya uwepo wa Mwenyezi Mungu ambaye atawasaidia kubomoa kuta za ubinafsi zinazochafua uhusiano kati ya watu na kati ya mataifa na hatimaye, kuibua ndani mwao hamu ya kutaka kujipatanisha, kusameheana na kudumisha amani hata kwa wale ambao wana moyo mgumu kama wa jiwe!

Baba Mtakatifu anawataka vijana kumtafuta muasisi wa tunu hizi msingi kwa kushirikiana na wenzi wao shuleni na katika michezo. Wasaidiane kumtafuta Muasisi mkuu wa maisha, furaha, upendo, amani, kwani hatimaye watagundua kwamba, yuko kati yao na huyu ndiye Mungu aliyejifanya mtoto katika Nafsi ya Yesu Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.