2012-12-19 09:09:49

Umaskini, ujinga, rushwa na ufisadi visiwalazimishe wananchi kukubali kukumbatia utamaduni wa kifo!


Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria limeonya dhidi ya Kampeni ya kudhibiti ongezeko la watu inayoendeshwa na Serikali pamoja na Mashirika ya Kimataifa nchini humo kwa kusema kwamba, Nigeria haina tatizo la ongezeko kubwa la watu kama wanavyodhani, kinyume chake ni kutaka kupandikiza mbegu ya utamaduni wa kifo ambayo madhara yake ni makubwa kwa siku za usoni.

Sera za uzazi salama ni hatari kwa ustawi na maendeleo ya nchi kwa siku za usoni anasema Askofu Gabriel Dunia, Mwenyekiti wa Tume ya Afya, Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria, alipokuwa anazungumzia kuhusu msimamo wa Kanisa Katoliki nchini Nigeria kuhusiana na masuala ya Familia pamoja na udhibiti wa vifo vya Wanawake Wajawazito nchini Nigeria. Umaskini, ujinga, rushwa na ufisadi visiwatumbukize watu katika janga kwa kukubali kutekeleza sera ambazo ni kinyume kabisa cha maadili na utu wema.

Nigeria inahitaji kuwa na viongozi wenye mipango thabiti, wanaoweza kutumia vyema rasilimali na utajiri wa nchi katika kupambana na changamoto mbali mbali zinazokwamisha maendeleo ya wananchi wa Nigeria. Kuna haja ya kuwa na mgawanyo sawa wa rasilimali ya nchi kwa ajili ya mafao ya wengi. Wananchi wanapaswa kuwa makini na sera zinazokumbatia utamaduni wa kifo sanjari na utoaji mimba.

Watu waelimishwe kuhusu mpango wa uzazi kwa njia asili, dhamana na wajibu wa wazazi katika maisha ya ndoa na familia ni kati ya mambo ambayo yanapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika masuala ya kifamilia badala ya kujikita katika kuhamasisha watu kukumbatia utamaduni wa kifo!







All the contents on this site are copyrighted ©.