2012-12-19 08:54:10

Maliasili na utajiri wa Sudan ya Kusini vitumike kwa ajili ya mafao ya wengi na maendeleo endelevu ya wananchi wa Sudan


Kardinali John Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, hivi karibuni alikuwa ni mgeni rasmi katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 100 ya Parokia ya Mupoi, iliyoko Sudan ya Kusini. Katika mahubiri yake ameonya kwamba, utajiri wa mafuta uliopo nchini Sudan, ukitumiwa vyema kwa mafao ya wengi, unaweza kuwa ni kichochea kikubwa cha maendeleo endelevu, lakini uzoefu unabainisha kuwa mara nyingine utajiri na rasilimali hizi zimekuwa ni chanzo cha vurugu, kinzani na vita.

Inasikitisha kuona kwamba, hata baadhi ya viongozi wa kitaifa waliotopea katika rushwa na ufisadi wanashirikiana na wawekezaji kutoka nje kwa ajili ya kuwapokonya wananchi utajiri ambao ungetumika kwa ajili ya mapambano dhidi ya ujinga, maradhi na umaskini katika nchi zao. Utajiri wa nchi hizi katika takwimu unaonesha kuwa ni mkubwa, lakini watu wake bado wanaendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini, ujinga na maradhi.

Ni changamoto kwa Serikali ya Sudan ya Kusini kuhakikisha kwamba, inatumia utajiri wake kwa ajili ya mafao ya wengi na maendeleo endelevu ya watu wake. Wananchi waendelee kushikamana, kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa, ili kwa pamoja waweze kukabiliana na changamoto za: utawala bora, mshikamano wa kitaifa, uzalendo na ukakamavu katika ujenzi wa taifa kwa umoja na upendo. Wananchi wa Sudan ya Kusini, wafahamiane, wapendane na kuheshimiana kama taifa moja.







All the contents on this site are copyrighted ©.