2012-12-18 15:34:38

Uchaguzi wa ANC, Rais Zuma aibuka kidedea!


Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini amechaguliwa kwa kishindo kuongoza tena cha ANC kwa kipindi kingine cha miaka mitano kwa kumshinda mpinzani wake Bwana Kgalema Motlanthe ambaye ni Makamu wa Rais Afrika ya Kusini. Rais Zuma amenyakua kura 2,983 dhidi ya mpinzani wake aliyejipatia kura 991.

Chama cha ANC kimemchagua pia Bwana Cyril Ramaphosa kuwa Makamu Mwenyekiti wa ANC. Huyu ni kati ya "vigogo" wenye utajiri wa kutisha nchini Afrika ya Kusini; utajiri unaokadiriwa kufikia kiasi cha $675 millioni.

Wajumbe wapatao 4,000 walikusanyika siku ya Jumanne tarehe 18 Desemba 2012 kuwachagua viongozi wao kwa kipindi kingine cha miaka mitano. Uchaguzi huu kadiri ya taarifa za vyombo vya habari umetanguliwa na vitisho na shutuma za rushwa, lakini hatimaye, ANC imemchagua Rais Jacob Zuma mwenye umri wa miaka 70 kuiongoza ANC. Afrika ya Kusini inaendelea kukabiliana na changamoto mbali mbali ikiwa ni pamoja na kudumisha mchakato wa ukweli na upatanisho; mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi ambao unagusa hata viongozi waandamizi wa Serikali ya Afrika ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.