2012-12-18 08:41:06

Kanisa linaomboleza na kumshukuru Mungu kwa ajili ya Marehemu Askofu mkuu Ambrose Madtha


Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, Jumatatu tarehe 17 Desemba 2012 aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumkumbuka na kumwombea Marehemu Askofu mkuu Ambrose Madtha, aliyekuwa Balozi wa Vatican nchini Pwani ya Pembe, aliyefariki kwa ajali ya gari tarehe 8 Desemba 2012 na kuzikwa Jimboni Mangalore, nchini India hapo tarehe 14 Desemba 2012.

Katika mahubiri yake, Kardinali Bertone alisema kuwa Kanisa linaomboleza kifo cha mtumishi wake Askofu mkuu Madtha, mtumishi mwaminifu na mkomavu, aliyetekeleza utume wake bila ya kujibakiza hata kidogo. Kanisa pia linamshukuru Mungu kwa zawadi ya Askofu mkuu Madtha ambaye kwa jicho na mwanga wa imani anapumzika mbele ya Mwenyezi Mungu baada ya kutekeleza wajibu wake, daima akiwa mwaminifu kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ni changamoto kwa kila mwamini kujiandaa, kukesha na kusali, daima taa za imani zikiwa zinawaka kwani hakuna anayejua siku wala saa atakapokuja Mwana wa Mtu, kama ambavyo kifo cha ghafla kilivyomfika Askofu Madtha. Dhana ya kukesha anasema Kardinali Bertone ni mwaliko wa kuendelea kutekeleza nyajibu mbali mbali kwa ajili ya kutangaza na kueneza Ufalme wa Mungu na utoaji wa huduma ya upendo kwa jirani katika uhuru kamili pamoja na kusikiliza Neno la Mungu.

Marehemu Askofu mkuu Madtha alijitoa kwa unyenyekevu mkuu kusaidia mchakato wa upatanishi miongoni mwa wananchi wa Pwani ya Pembe waliojikuta wakiogelea katika misigano na kinzani za kisiasa na kivita. Ni kiongozi aliyependelea kujikita katika majadiliano ya kina kwa ajili ya mafao ya wengi. Kwa kushirikiana na Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe, ameisaidia Familia ya Mungu kutekeleza wajibu wake barabara katika utoaji wa huduma: kiroho na kimwili.

Marehemu Askofu mkuu Ambrose Madtha alizaliwa huko Belthangady, India, kunako tarehe 2 Novemba 1955. Akapadrishwa kunako tarehe 28 Machi 1982. Akaanza huduma na utume wa Kidiplomasia mjini Vatican mwaka 1990, huko Ghana, El Salvadoro, Georgia, Albania na China.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, tarehe 8 Mei 2008 akamteua kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Pwani ya Pembe, utume ambao ameutekeleza kwa kipindi cha miaka minne, akiwa bega kwa bega na Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe katika utekelezaji wa mikakati mbali mbali ya maisha na utume wa Kanisa nchini humo.







All the contents on this site are copyrighted ©.