Akaunti ya Papa @ Pontifex ina wafuasi zaidi ya millioni mbili!
Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano anasema kwamba,
hadi sasa kuna zaidi ya wafuasi millioni mbili ambao wako tayari kwenye akaunti ya
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwenye mtandao wa Twitter, tangu ulipozinduliwa
rasmi hapo tarehe 12 Desemba 2012.
Mitandao ya Kijamii ni Jukwaa linalokusanya
umati mkubwa wa watu wanaoishi katika ulimwengu wa mitandao ambao hadi sasa idadi
yao inakadiriwa kufikia millioni mia moja na arobaini. Hili ni kundi la vijana wenye
umri kati ya miaka kumi na nane hadi thelathini na nne wanaounda asilimia arobaini
ya watumiaji wa mitandao ya Kijamii. Haya ni matunda ya maendeleo ya sayansi na teknolojia
ya habari yanayowawezesha watu kuwasiliana kwa haraka zaidi. Ni Jamii yenye utamaduni
na vipaumbele vyake na kwamba haya ni maskani mapya ya maisha ya binadamu yanayopaswa
Kuinjilishwa.
Si haba ndiyo maana hata Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita, ameamua kujiunga na mitandao ya kijamii ili kuwashirikisha watumiaji wa mitandao
hii kweli za Kiinjili, hata kwa ujumbe mfupi kabisa. Hapa kinachotakiwa si wingi wa
maneno, bali maudhui yaliyomo kwenye maneno haya.
Kanisa linatambua fika uwezo
na mapungufu yaliyomo kwenye mitandao ya kijamii. Ni maendeleo ambayo yanagusa sehemu
ya watu duniani, lakini katika maeneo kama Bara la Afrika, Amerika ya Kusini na baadhi
ya mataifa ya Asia, maendeleo haya yanagusa kundi dogo sana la watu kutokana na sababu
mbali mbali. Kutokana na changamoto kama hizi, Kanisa litaendelea kutumia njia mbali
mbali ili kuhakikisha kwamba, watu wanakutana na Habari Njema ya Wokovu pale walipo.
Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari na mawasiliano imeiwezesha Jamii
kupata habari nyingi kwa wakati mmoja, kiasi kwamba, wakati mwingine watu wanajikuta
wakichanganyikiwa kutokana na mafuriko ya habari zinazowafikia kwa muda mfupi kabisa.
Madhara kama haya yanaweza kuwafanya watu kupoteza ladha na utamu wa Injili inayozima
kiu na matamanio ya binadamu kutoka katika undani wa maisha yake.
Askofu mkuu
Claudio Maria Celli anabainisha kwamba, hili ni tatizo na changamoto zinazopaswa kufanyiwa
kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo ili kuhakikisha
kuwa watu wanaelimishwa kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii, kwa maneno
mengine hata Jukwaa la mitandao ya kijamii linapaswa Kuinjilishwa ili kujikita zaidi
katika kutafuta mafao ya wengi na maendeleo endelevu ya mwanadamu.