2012-12-17 08:45:55

Watanzania achaneni na kilimo cha Jembe la Mkono hakina tija!


Waziri Mkuu Mizengo Pinda wa Tanzania amesema, wilaya mpya ya Mlele mkoani Katavi itakuwa na Halmashauri mbili za Mlele na Nsimbo ili kurahisisha utoaji huduma kwa wananchi. Ametoa kauli hiyo Jumamosi, Desemba 15, 2012, wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Inyonga kwenye viwanja vya shule ya msingi Inyonga akiwa katika siku ya tatu ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi.
Aliwaeleza wakazi hao kwamba Rais Jakaya Kikwete aliamua kuwapa wilaya mpya na mkoa mpya kwa ili kuleta maendeleo kwa haraka. “Rais Kikwete alifanya hivyo kwa sababu alijua kwamba rasilmali zikiletwa Rukwa (mkoa wa zamani) hadi zifike hapa Mlele zitakuwa ni kidogo sana,” alisema. Kufuatia mgawanyo huo, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele itakuwa na kata 13 ambazo ni Ilunde, Ilela, Nsenkwa, Inyonga, Utende, Kasanga na Mamba. Nyingine ni Majimoto, Mwamapuli, Mbede, Usevya, Itenka na Kibaoni.
Nayo Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo itakuwa na kata 11 ambazo ni Ugalla, Uruira, Kasokola, Mtapenda, Nsimbo na Sitalike. Nyingine ni Kapalala, Machimboni, Litapunga, Itenka na Magamba. Ili kuendana na kasi ya mabadiliko, Waziri Mkuu aliwataka wakazi hao wachangamkie fursa zilizopo kwa kuachana na kilimo cha matuta. Aliwataka mabwana shamba waandae mashamba darasa kwa kila kijiji ili wananchi waweze kujifunza kwa mifano.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu ameahidi kutoa miche 1,000 ya miembe ya kisasa kwa vijana wa vijiji vya Uruira na Usense wilayani Mlele kama njia ya kuwahamasisha walime mazao mbadala. Alitoa ahadi Jumamosi jioni, Desemba 15, 2012), wakati akizungumza na wakazi wa vijiji hivyo kwenye viwanja vya shule ya msingi Uruira katika kata ya Uruira wakati akiwa njiani kurejea Mpanda mjini.
“Nimemwambia Mkuu wa Mkoa (Dk. Rajab Rutengwe) ahamasishe kilimo cha maembe ya kisasa... yale ni makubwa ili muachane na haya madogo ya kwenu. Vijana hawa wapeni eneo na nitawaletea miche 1,000 ya maembe ya kisasa kwa kuanzia,” alisema. Akihimiza kanuni bora za kilimo, Waziri Mkuu ambaye ni mbunge wa Jimbo la Mlele aliwataka waachane na kilimo cha matuta na badala yake watumie kilimo cha sesa.
“Ekari moja ya mahindi inapaswa iwe na miche 16,000 ili ikupatie magunia 20-25 ya mahindi, sasa wewe unalima ekari tatu na kuvuna magunia 10, sababu kubwa ni nafasi zinazopotea kwenye miraba ya matuta, alisema. “Ni lazima tuondokane na kilimo hiki kwa sababu hakina tija na tena kinatumia nguvu nyingi na kupoteza eneo kubwa ambalo lingetumika kupanda mazao,” alisisitiza.








All the contents on this site are copyrighted ©.