Watanzania achaneni na kilimo cha Jembe la Mkono hakina tija!
Waziri Mkuu Mizengo Pinda wa Tanzania amesema, wilaya mpya ya Mlele mkoani Katavi
itakuwa na Halmashauri mbili za Mlele na Nsimbo ili kurahisisha utoaji huduma kwa
wananchi. Ametoa kauli hiyo Jumamosi, Desemba 15, 2012, wakati akizungumza na wakazi
wa kata ya Inyonga kwenye viwanja vya shule ya msingi Inyonga akiwa katika siku ya
tatu ya ziara yake jimboni kwake Katavi wilayani Mlele, mkoani Katavi. Aliwaeleza
wakazi hao kwamba Rais Jakaya Kikwete aliamua kuwapa wilaya mpya na mkoa mpya kwa
ili kuleta maendeleo kwa haraka. “Rais Kikwete alifanya hivyo kwa sababu alijua kwamba
rasilmali zikiletwa Rukwa (mkoa wa zamani) hadi zifike hapa Mlele zitakuwa ni kidogo
sana,” alisema. Kufuatia mgawanyo huo, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele itakuwa na kata
13 ambazo ni Ilunde, Ilela, Nsenkwa, Inyonga, Utende, Kasanga na Mamba. Nyingine ni
Majimoto, Mwamapuli, Mbede, Usevya, Itenka na Kibaoni. Nayo Halmashauri ya Wilaya
ya Nsimbo itakuwa na kata 11 ambazo ni Ugalla, Uruira, Kasokola, Mtapenda, Nsimbo
na Sitalike. Nyingine ni Kapalala, Machimboni, Litapunga, Itenka na Magamba. Ili kuendana
na kasi ya mabadiliko, Waziri Mkuu aliwataka wakazi hao wachangamkie fursa zilizopo
kwa kuachana na kilimo cha matuta. Aliwataka mabwana shamba waandae mashamba darasa
kwa kila kijiji ili wananchi waweze kujifunza kwa mifano. Wakati huohuo, Waziri
Mkuu ameahidi kutoa miche 1,000 ya miembe ya kisasa kwa vijana wa vijiji vya Uruira
na Usense wilayani Mlele kama njia ya kuwahamasisha walime mazao mbadala. Alitoa ahadi
Jumamosi jioni, Desemba 15, 2012), wakati akizungumza na wakazi wa vijiji hivyo kwenye
viwanja vya shule ya msingi Uruira katika kata ya Uruira wakati akiwa njiani kurejea
Mpanda mjini. “Nimemwambia Mkuu wa Mkoa (Dk. Rajab Rutengwe) ahamasishe kilimo
cha maembe ya kisasa... yale ni makubwa ili muachane na haya madogo ya kwenu. Vijana
hawa wapeni eneo na nitawaletea miche 1,000 ya maembe ya kisasa kwa kuanzia,” alisema.
Akihimiza kanuni bora za kilimo, Waziri Mkuu ambaye ni mbunge wa Jimbo la Mlele aliwataka
waachane na kilimo cha matuta na badala yake watumie kilimo cha sesa. “Ekari moja
ya mahindi inapaswa iwe na miche 16,000 ili ikupatie magunia 20-25 ya mahindi, sasa
wewe unalima ekari tatu na kuvuna magunia 10, sababu kubwa ni nafasi zinazopotea kwenye
miraba ya matuta, alisema. “Ni lazima tuondokane na kilimo hiki kwa sababu hakina
tija na tena kinatumia nguvu nyingi na kupoteza eneo kubwa ambalo lingetumika kupanda
mazao,” alisisitiza.