Wajibu na dhamana ya Familia za Kikristo katika kulinda, kutetea na kudumisha utamaduni
na ustaarabu unaoheshimu utu, maadili na dhamiri nyofu
Kardinali Vingt-Trois, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa, hivi karibuni
amezungumzia kuhusu ndoa na umuhimu wa familia katika maisha ya kijamii, kama njia
ya kuanzisha mchakato unaopania kujenga ustaarabu mpya unaojikita katika mapendo thabiti
kati ya mwanaume na mwanamke.
Amegusia hali
halisi ya maisha ya ndoa na familia nchini Ufaransa, yanayoendelea kubadilika kwa
kasi ya ajabu. Utu na heshima ya mwanadamu havina tena kipaumbele cha kwanza katika
mabadiliko haya. Mwenyezi Mungu katika busara yake, alimuumba mwanamume na mwanamke,
ili waweze kutegemezana na kukamilishana na kwa njia hii, waweze kuendeleza ile kazi
ya uumbaji ambayo alimkabidhi mwanadamu, tangu kuumbwa kwa msingi wa ulimwengu.
Tangu
mwanzo wa mapokeo ya Kiyahudi na Kikristo ndoa imekuwa ikiheshimiwa kutokana na utakatifu
wake. Ni kwa njia ya ndoa, Mwenyezi Mungu alifunga agano na mwanadamu, ili kuendeleza
ile kazi ya uumbaji inayofanywa na wazazi yaani Bwana na Bibi na wala si vinginevyo!
Mtoto ni zawadi na tunda la uhusiano wa dhati kati ya Bwana na Bibi. Mwelekeo wa kupendana
kati ya watu wa jinsia mbili tofauti ni sehemu ya mpango wa Mungu unaofanyika kwa
kuzingatia uhuru wa watu husika pasi na shuruti.
Muungano kati ya Bwana na
Bibi ndani ya Kanisa unaitwa Sakramenti inayowapatia watu hawa dhamana na wajibu mbele
ya Kanisa na Jamii. Wanapaswa kutambua kwamba, ni muungano wa kudumu, hadi pale kifo
kitakapowatenganisha kadiri ya mpango wa Mungu. Wanandoa wanaweza kuwa ni vyombo
vya kudumisha haki, amani na utulivu ndani ya Jamii, ikiwa kama kila upande utatekeleza
wajibu wake barabara.
Familia iwe ni mahali ambapo watoto wanajifunza tunu
bora za maisha ya kiroho, kiutuu, kijamii na kitamaduni. Ni nguzo thabiti ya Jamii
katika utekelezaji wa majukumu yake ya malezi na majiundo makini. Ndani ya Familia,
watoto wanapaswa kupendwa na kuthaminiwa kama walivyo! Kuna uhusiano wa pekee kabisa
kati ya wazazi na watoto wao unaobubujika katika maisha ya kibayolojia. Hapa ni kielelezo
cha mshikamano wa dhati kati ndani ya Familia unaozaa maisha kama zawadi inayopaswa
kupokelewa na kuthaminiwa.
Kardinali Vingt-Trois anasema, upendo wa maisha
ya ndoa ni kielelezo cha pekee kabisa cha agano kati ya Mungu na watu wake. Manabii
walitumia lugha ya upendo wa maisha ya ndoa, kuelezea upendo ambao Mwenyezi Mungu
aliuonesha kwa watu wake na hatimaye, kuthibitishwa na Kristo aliyeanzisha Sakramenti
ya Ndoa kwa ajili ya Kanisa lake. Mwanaume na mwanamke wanashiriki katika agano na
Mwenyezi Mungu.
Ikiwa kama mwanadamu anataka kufuta dhana hii, kwa hakika
hatekelezi ule mpango wa Mungu kwa maisha na ustawi wa mwanadamu. Upendo wa kibinadamu
ni kielelezo cha upendo wa Mungu kwa mwanadamu, kiini na chemchemi ya Familia mintarafu
Mafundisho ya Kanisa. Mabadiliko ya sheria za nchi zinazoruhusu watu wa jinsia moja
kuoana ni jambo nyeti kabisa kwani linagusa undani na uhuru wa Mungu na binadamu katika
ujumla wao.
Ni kielelezo cha mmong’onyoko wa maadili na utu wema. Kanisa linaposimama
kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, linajikita zaidi
katika uzazi na dhamana ya kuendeleza kizazi sanjari na dhamana ya watoto ndani ya
Jamii. Kanisa linapinga uzalishaji wa watoto kwa njia ya maabara kwani linapenda wazazi
kuwajibika barabara katika tendo la ndoa ambalo ni takatifu na lina umuhimu wa pekee
kwa wanandoa wenyewe.
Kardinali Vingt-Trois anasema, Kanisa halina mpango wa
kuendesha vita vya kisiasa dhidi ya sera zinazotaka kuleta mabadiliko kwa ajili ya
kutetea asilimia mbili ya watu wanaounga mkono ndoa za watu wa jinsia moja. Kanisa
linasukumwa na dhamiri nyofu, utu na heshima ya mwanadamu, linawaalika waamini na
watu wenye mapenzi mema, kusimama kidete kutoa mawazo ya dhidi ya utamaduni unaotaka
kupinga mpango wa Mungu.
Watu wanapenda kukumbatia mno malimwengu na kwamba,
Familia kwa sasa inaonekana kuwa ni kero kwa baadhi ya watu! Ni wajibu wa Familia
za Kikristo kusimama kidete kulinda na kutetea tunu bora za maisha ya kifamilia ili
kudumisha utamaduni na ustaarabu unaoheshimu utu, maadili na dhamiri nyofu.