2012-12-17 13:53:28

Kanisa linatambua na kuthamini michezo kama sehemu ya majiundo makini, mahali pa kutambua na kuthamini zawadi ya maisha na kusikiliza kwa makini!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatatu tarehe 17 Desemba 2012 alikutana na kuzungumza na Kamati ya Michezo ya Olimpic ya Kitaifa, Italia, iliyoshiriki hivi karibuni katika michezo ya Olimpic iliyohitimishwa mjini London, 2012 kwa kuwashirikisha wanamichezo kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kama mahali pa ushindani wa ufundi, uwezo na karama ambazo walizitumia ili kufanikisha mashindano hayo, pamoja na kutambua uwezo wao unapoishia.

Baba Mtakatifu anawapongeza kwa ushindi mkubwa waliojipatia wakati wa Mashindano ya Olimpic, kielelezo cha nidhamu ya hali ya juu inayoheshimu mwili wa mwanadamu, kwa kuonesha pia mshikamano, furaha na mafanikio yaliyogeuzwa kuwa ni sherehe ya wengi. Hiki ni kielelezo cha ukuaji wa binadamu, kwa kujikatalia, kwa kujenga na kudumisha moyo wa uvumilifu, unyenyekevu ambao kimsingi ndiyo siri ya ushindi ya wanamichezo.

Michezo haina budi kuonesha huduma kwa mwanadamu, kwa kuheshimu sheria na kanuni za michezo, uelewa na mtazamo wa binadamu anayehitaji kwa namna ya pekee, elimu, maisha ya kiroho na tunu msingi zinazovuka upeo wake wa kibinadamu. Michezo ni fursa makini ya elimu na utamaduni inayomwezesha mwanadamu kujifahamu na hatimaye, kufahamu maana ya maisha yake. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanabainisha kwamba, michezo ni mahali ambapo mwanadamu anafafanua maana ya maisha, utu na uhusiano wake na wengine.

Hapa ni mahali pa mwanadamu kufanya maboresho ya maisha yake, anajitajirisha kwa kufahamiana na wengine, kwa kusaidiana pamoja na kuweka uwiano mzuri wa utu wake unaopania kujenga na kuimarisha uhusiano wa kidugu kati ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Utamaduni wa michezo unajengeka katika utu wa mtu, ni sehemu ya huduma kwa mwanadamu na wala si vinginevyo.

Mama Kanisa anatambua na kuthamini mchango wa michezo kama sehemu ya elimu, majiundo makini ya mtu, uhusiano pamoja na tasaufi, ndiyo maana Kanisa linatoa kipaumbele cha kwanza kwa michezo katika viwanja vya Parokia zake; mahali pa kujifunza na kujenga udugu, kutambua na kuthamini zawadi ya maisha; daima wakiwa makini kuthamini mpango wa Mungu katika maisha na kusikiliza kwa umakini mkubwa nyakati za mazoezi.

Mazoezi yanaweza kuwa ni fursa ya kujibu maana ya maisha. Michezo inamfunda mtu tunu msingi za maisha ya kiutu, changamoto kwa wadau wa michezo kutolea ushuhuda wa tunu hizi wanazozimwilisha katika michezo; kwa kushirikiana na familia na taasisi za malezi na majiundo ya vijana bila kuwasahau wadau wengine katika michezo.

Kamwe wanamichezo wasitafute njia ya mkato kwa kutumia madawa ya kuongeza nguvu; wale wanaoteleza na kuangukia katika mawazo haya duni, wapokelewe na kusaidiwa. Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, iwe ni fursa kwa wanamichezo kujifunza pia mapambano ya maisha ya kiroho, kwa kuhakikisha kwamba, wema unashinda ubaya; ukweli unatawala dhidi uwongo; upendo dhidi yachuki na uhasama. Michezo iwe ni uwanja wa majadiliano ya kidini na wale wanaoamini na wale wasioamini; pawe ni mahali pa kushirikishana furaha na magumu ya maisha kwa watu kutoka katika tamaduni, lugha na mielekeo ya mbali mbali ya kidini.

Kuwa Mkristo ni kupenda zawadi ya maisha, mazingira pamoja na kuwapenda jirani, hasa wale wanaokabiliana na hali ngumu ya maisha. Baba Mtakatifu amehitimisha hotuba yake kwa kuwatakia wajumbe wa Kamati ya Olimpic Italia na wanamichezo wote kheri na baraka kwa Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2012.







All the contents on this site are copyrighted ©.