2012-12-17 10:57:16

Jubilee ya miaka 100 ya Imani Katoliki Kaskazini mwa Uganda ni changamoto ya kuendelea kujishikamanisha na Kristo kwa njia ya ushuhuda makini!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu amehitimisha hija yake ya kichungaji nchini Uganda kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee ya Miaka Mia Moja ya Imani Katoliki, Kaskazini mwa Uganda, kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa wema na ukarimu aliowajalia waamini wa Kanisa Katoliki Uganda. Huu ni mchango wa Taifa la Mungu katika kurithisha Imani ya Kanisa Katoliki kutoka kizazi hadi kizazi, wakitekeleza agizo la Yesu kwenda duniani kote ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu.

Tangu wakati huo, waamini Kaskazini mwa Uganda walipokea imani iliyoletwa kwao kwa njia ya Wamissionari, wakiimwilisha katika maisha na kuvirithisha vizazi vingine vilivyofuata kwa njia ya Ibada. Huu ni mchako mkubwa uliotolewa na Makatekista waliokuwa ni wasaidizi wakuu wa Wamissionari katika utekelezaji wa dhamana ya Uinjilishaji. Kuna wafuasi mbali mbali wa Kristo ambao wameonesha ushuhuda wa pekee kwa njia ya maisha yao na kwamba, kwa damu yao imekuwa ni chemchemi ya Ukristo nchini Uganda.

Changamoto kubwa inayowakabili waamini sehemu mbali mbali za dunia ni kuchuchumalia wongofu wa ndani na utakatifu wa maisha kama wanavyohimiza Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Mababa wa Sinodi ya Uinjilishaji Mpya iliyohitimishwa hivi karibuni mjini Vatican. Waamini wajitahidi kujipatanisha wao kwa wao pamoja na Mwenyezi Mungu kama njia mpya ya uinjilishaji Mpya unaodai toba na wongofu wa ndani.

Kardinali Filoni anaitaka Familia ya Mungu nchini Uganda kuimarisha Katekesi kuhusu Sakramenti za Kanisa, hasa Ubatizo, Ekaristi takatifu na Kipaimara; Sakramenti ambazo zinamwingiza mwamini katika Ukristo, tayari kuanza hija ya utakatifu wa maisha. Kanisa nchini Uganda liendelee kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa wale ambao bado hawajabahatika kuisikia na waamini waendelee pia kuyatakatifuza malimwengu kwa kuonesha ushuhuda wa kukutana na Yesu anayewakirimia furaha tele katika imani.

Familia ya Mungu iendelee kuwajibika kwa kuwatunza na kuwasaidia waathirika wa Ugonjwa wa Ukimwi; wahanga wa vita na ubaguzi kwa kuwaoneasha kwamba, wana upendeleo wa pekee machoni pa Kristo. Katika utekelezaji wa dhamana ya Uinjilishaji Mpya, wakumbuke kwamba, hawako peke yao, kwani Kristo ameahidi kuwa pamoja nao hadi ukamilifu wa dahali. Maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia moja ya Ukristo Kaskazini mwa Uganda iwe ni fursa ya kujishikamanisha na Kristo katika adhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu; wajitoe kimaso maso kutangaza Habari Njema ya Wokovu ndani na nje ya mipaka ya Uganda.

Bikira Maria nyota ya Uinjilishaji Mpya awalinde na kuwaongoza katika utekelezaji wa Uinjilishaji Mpya. Ni mwaliko wa Majimbo ya Nebbi, Gulu, Lira na Arua kusimama kidete ili kutangaza matendo makuu ya Mungu katika maisha na utume wao nchini Uganda.







All the contents on this site are copyrighted ©.