2012-12-17 08:20:29

Dhamana na majukumu ya wanawake katika maisha na utume wa Familia


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican katika kipindi chetu kilichopita tuligusia kuhusu uwiano wa majukumu ya kiuchumi na malezi katika familia kati ya mume na mke. Tulimalizia kusema mwanamume anapofanya kazi za kiuchumi nje ya familia awe na lengo la kuipatia familia yake mkate au mahitaji yake ya kila siku. RealAudioMP3
Hata hivyo ongezeko la mahitaji ya leo lililoletwa na mabadiliko ya kiuchumi linaonyesha kuwa ajira ya baba pekee yake haitoshi kwa mahitaji yote ya familia. Hivyo leo tunashudia alama wazi kuwa mwanamke naye hana njia nyingine ila kujiingiza kwenye shughuli za ajira na kiuchumi.
Tendo hili halina ubaya wowote ila tunarudia tena kusema mwanamke ni mama wa watoto lakini mke kwa mumewe. Kazi yoyote ya kiuchumi isije ikamtoa kwenye majukumu haya, isije ikahatarisha umoja wa kindoa na kuwa pingamizi katika uzazi na makuzi ya watoto ambayo kwa hakika mwanamke ndiye muhimili mkuu.
Kwa bahati mbaya wimbo la kiuchumi, kisiasa, kijamii na hata wimbo la haki sawa kwa mwanamke linawafanya wanawake wengi watamani na hata kufanya kila njia kujivua uanawake wao katika majukumu ili wapate elimu ya juu, kipato cha juu na nafasi za juu katika ajira huku wakitupilia mbali uzazi na malezi. Ni masikitiko makubwa kuwa nchi zilizoendelea zimejikuta kwenye idadi ndogo ya watoto yaani kundi tegemezi.
Kiuchumi inaonekana ni sawa kwani ndio maendeleo lakini baadaye ya taifa iko wapi bila watoto? Baadhi ya mataifa yaliyoendelea yamesituka na kuanza kampeni ya kuelimisha kuhusu umuhimu wa uzazi ila kwa kuchelewa na sio kazi rahisi kutibu ugonjwa wa fikira.
Nasikitika mitaala ya kufundishia mashule ya nchi zetu zinazoendelea sasa inakazia kwamba njia sahihi ya kuondokana na ogezeko la watu na hasa kundi tegemezi ni kupunguza uzazi hata kwa njia za mauaji. Je, nasi hatajikuta kwenye hali kama hiyo? Maendeleo ya kichumi sawa lakini kuwe na uwiano kati ya uchumi na familia na hasa nafasi ya mwanamke ambaye ndiye anayebeba mimba na kuzaa.
Jambo la msingi katika familia ni upendo na ushirikiano. Mume, mke na watoto ni zawadi na tiba ya kisaikolojia kila mmoja kwa mwingine. Wakati wote wana- familia wajitahidi kujenga mazingira ya furaha pamoja. Ikumbukwe pia kuwa, familia ni zawadi kwa jamii nzima kwani ndio wanaounda jamii na ndio wateja wa haki, amani na majukumu ya jamii nzima kumbe jamii katika maana ya serikali isaidie ustawi wa familia.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Raphael Mwanga, wa Jimbo Katoliki la Same, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa Laterano- Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.