2012-12-15 09:20:05

Miaka 40 ya WAWATA imekuwa ni ya Utumishi wa upendo kwa vitendo!


Askofu Desiderius Rwoma, Mwenyekiti wa Idara ya Walei, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, TEC, anawapongeza Wanawake Wakatoliki Tanzania wanapoadhimisha Miaka 40 ya utumishi kwa vitendo. Kipindi hiki kuanzia mwaka 1972 hadi mwaka 2012 ni safari ndefu ya kujitakasa, kujiandaa na kutekeleza wajibu. Kutujuvya zaidi ni Padre Agapito Mhando. RealAudioMP3

Ni kipindi cha matumaini ya kusonga mbele licha ya magumu na changamoto nyingi. Ni kipindi cha kukua na kukomaa katika: Imani, Matumaini na Mapendo, daima wakiendelea kumtegemea Mwenyezi Mungu kama walivyofanya Waisraeli katika hija yao ya miaka arobaini Jangwani. Ni mwaliko wa kufanya toba na kuchuchumilia wongofu wa ndani, ili kupata neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Miaka 40 ya WAWATA, kimekuwa ni kipindi cha huduma kwa Familia ya Mungu nchini Tanzania. Wengi wameguswa na utume wa WAWATA wanaoendelea kutumikia na kuwajibika kwa upendo wa Kristo. Ni wanawake wanaokubali, kuthamini, kulinda na kutetea Injili ya uhai; kwa kulea, kushauri na kuelekeza watoto wao katika kuchagua miito mbali mbali ndani ya Kanisa.

WAWATA imekuwa mstari wa mbele katika kuwategemeza Waseminari na kuendelea kutangaza Injili ya Upendo kwa wahitaji na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha. Kwa hakika, miaka arobaini ya WAWATA imekuwa ni Injili kwa vitendo. Vita wameipiga, Imani wameilinda, lakini mwendo bado hawajaumaliza, kwani utume wao bado unahitajika kwa ajili ya wokovu wao binafsi na ulimwengu katika ujumla wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.