2012-12-14 09:52:06

Unaweza kuishi vyema Mwaka wa Imani: kwa njia ya Sala, Tafakari ya Neno la Mungu na Matendo ya Huruma!


@Pontifex, ndiyo akaunti ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika mtandao wa kijamii unaojulikana kama Twitter, ambao siku ya kwanza ya kuzinduliwa kwake, Jumatano, tarehe 12 Desemba 2012, saa 6: 00 umekwishapata wafuasi zaidi ya millioni moja. Baba Mtakatifu alitumia fursa hii kujibu maswali makuu matatu yaliyochaguliwa kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Swali la kwanza liliuliza ni kwa jinsi gani mwamini anaweza kuadhimisha vyema Mwaka wa Imani katika maisha yake ya kila siku? Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita akasema "ni kwa kuzungumza na Yesu katika Sala, kusikiliza kwa makini anayomwambia kutoka katika Injili na kumtafuta kati ya wenye shida". Kwa maneno mengine tungeweza kusema, mwamini anaweza kuishi vyema Mwaka wa Imani kwa njia ya Sala, Tafakari ya Kina ya Neno la Mungu na Matendo ya huruma.

Swali la pili liliuliza, Je, ni kwa jinsi gani Imani kwa Yesu inaweza kumwilishwa katika ulimwengu usiokuwa na matumaini? Baba Mtakatifu anajibu kwa kusema kwamba, mwamini akumbuke kwamba, hayuko peke yake. Mwenyezi Mungu ni mwamba thabiti ambao mwamini anajenga maisha juu yake na upendo wake daima ni amini.

Swali la tatu aliloulizwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Je, ni ushauri gani unaoweza kuutoa ili mtu aweze kuzama katika sala wakati ambapo amesongzwa na mambo ya kazi, familia na malimwengu? Baba Mtakatifu anajibu kwa kusema kwamba "Yatolee kwa Mungu yote unayofanya, omba msaada wake katika maisha yako ya kila siku na kumbuka kwamba, yuko daima pamoja nawe".







All the contents on this site are copyrighted ©.