Ujenzi wa nyumba za gharama nafuu waanza Dar Es Salaam
Ifuatayo ni hotuba ya Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania wakati wa kuweka jiwe la msingi
kuzindua ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, Dar es Salaam,hapo tarehe 13 Desemba 2012.
Namshukuru
sana Mheshimiwa Prof. Anna Tibaijuka, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi,
Ndugu Kesogukewele Msita, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Nyumba
na Ndugu Nehemia Mchechu, Mkurugenzi Mkuu wa NHC na uongozi wote wa Shirika kwa kunialika
kuja kushiriki katika tukio hili la kihistoria la kuweka jiwe la msingi la ujenzi
wa nyumba za gharama nafuu zinazojengwa na Shirika hapa Kibada.
Nawapongeza
Bodi na Menejimenti ya Shirika kwa kubuni wazo hili zuri na kulitekeleza. Mmefanya
uamuzi wa busara wa kujenga nyumba hizi kwa ajili ya watu wenye kipato cha kawaida.
Uamuzi huu wa kizalendo unatoa taswira nzuri ya Shirika kwa jamii na kujenga imani
miongoni mwa watu kuwa Shirika hili ni lao na lipo kwa ajili yao. Shirika sasa linajali
hata maslahi ya watu wenye kipato cha chini na cha kati. Hii ndiyo ilikuwa lengo
kuu la kuanzishwa kwa Shirika la Nyumba mara baada ya Uhuru. Hili mnalofanya leo
ndilo hasa jukumu lenu la msingi. Hongereni sana na naomba muendelee kufanya kazi
hii mliyoianza. Ndugu Wananchi;
Wananchi kuwa na nyumba bora za kuishi ni
moja ya malengo makuu ya Serikali tangu uhuru wa nchi yetu miaka 51 iliyopita mpaka
sasa. Ni hivyo, kwa sababu kuwa na nyumba ni mahitaji ya msingi ya mwanadamu. Lakini
pia Serikali ililazimika kusisitiza kuwa na nyumba bora kwa sababu wananchi wengi
walikuwa wanaishi katika nyumba za makuti. Hivyo basi Shirika lilianzishwa kuwasaidia
na kuwawezesha wananchi kuondoka kwenye nyumba za makuti na kuwa na nyumba bora.
Ndiyo siri ya kujengwa na kuwepo kwa nyumba nyingi za “neshnali” Magomeni, Kinondoni,
Mwananyamala, Ilala, Temeke, Mburahati, Buguruni na Keko kwa hapa Dar es Salaam na
kwingineko nchini.
Nyumba hizo nzuri na imara zilijengwa na kuuzwa kwa gharama
nafuu na watu wengi wenye kipato cha kawaida waliweza kumudu kuzinunua. Mpaka leo
nyumba hizo zipo, tena bado imara kabisa licha ya kuwa na umri unakaribia miaka 50.
Kwa bahati mbaya kasi ya Shirika ya kujenga nyumba mpya za namna hiyo
ilipungua hasa kuanzia miaka ya themanini kutokana na uhusiano wa nchi yetu na Ujerumani
kutetereka na uchumi wa nchi kupata misukosuko kuanzia miaka ya 1970. Na baada ya
nyumba za Msajili kukabidhiwa NHC, Shirika likasahau ujenzi wa nyumba. Shirika likabaki
na kazi ya kukusanya kodi ya pango kwenye nyumba ilizojenga na zile zilizokuwa za
Msajili. Kadri muda ulivyokuwa unakwenda Shirika likasahau kabisa wajibu wake wa
kujenga nyumba. Lakini, si hivyo tu, hata makusanyo ya kodi pia yakaanza kudorora
na uwezo wa kujiendesha wa Shirika ukapungua sana.
Hali hiyo, imekuwa
mtihani mkubwa kwa Serikali kuhusu haja ya kulirejesha Shirika katika hali nzuri.
Baadae Shirika likazinduka na kuanza tena ujenzi wa nyumba, lakini nyumba zake ni
ghali sana ambazo watu wa kipato cha kawaida hawazimudu. Kwa kweli Watanzania wengi
walioajiriwa hawazimudu hata wale wa vyeo vya juu, kwa vile mishahara yao bado si
mikubwa. Bahati mbaya pia hapakuwepo na utaratibu wa mikopo ya nyumba baada ya kufa
kwa Tanzania Housing Bank (THB) na mpango wa mikopo ya nyumba kwa watumishi wa umma. Ndugu
wananchi;
Kufuatia hali hiyo Serikali ikaamua kuchukua hatua za makusudi kuboresha
Shirika na kuhuisha Sera na Sheria zinazohusu uendelezaji wa sekta ya nyumba ili ziendane
na hali halisi ya wakati huu. Miongoni mwa hatua hizo ni kupata Bodi mpya na Mkurugenzi
mpya. Pia, kutungwa kwanza kwa Sheria ihusuyo mikopo ya nyumba ili watu waweze kupata
mikopo ya kujenga au kununua nyumba. Pili ni kutungwa kwa Sheria ya kuwezesha watu
kuuziwa nyumba mojawapo katika ghorofa lenye nyumba nyingi na kupewa hati ya kumiliki
nyumba hiyo. Utekelezaji wake umeanza, unaendelea ingawaje sijaridhika sana na kasi
ya utekelezaji wa Sheria hizi mbili.
Pamoja na hayo, ujenzi wa nyumba unaendelea
kwa kasi kubwa kote nchini kama tunavyoona wote. Hata hivyo, nyumba hizo ni ghali,
watu wenye vipato vya chini na wafanyakazi si rahisi kumudu. Wengine hushawishika
kufanya mambo yasiyostahili.
Nimefurahishwa sana na uamuzi wa Shirika
la Nyumba la Taifa kwa uamuzi wake wa kujenga nyumba za gharama nafuu. Mmerejea kwenye
madhumuni ya awali ya kuwepo kwenu. Sasa Shirika la Nyumba linafanya yale ambayo
ilitumwa kufanya tangu kuasisiwa kwake.
Nimesikia kilio chenu kuhusu kodi
ya ongezeko la thamani; bei za viwanja n.k. Wahusika wataambiwa. Pia, angalieni
uwezekano wa kuwakopesha wafanyakazi kwa masharti ya kudhaminiwa na waajiri wao kuwalipa
moja kwa moja.
Nashauri NHC nayo iangalie uwezekano wa kushiriki katika kuanzisha
benki ya nyyumba au kuwa na hisa katika benki zilizopo. Kukiwa na utaratibu wa mikopo
hususan yenye riba nafuu, wateja wa kununua nyumba watakuwa wengi na Shirika litanufaika.
Mtajenga nyumba za gharama nafuu na wanunuzi watakuwapo.
Nawapongeza sana
viongozi na watumishi wa Shirika kwa kazi nzuri muifanyao. Shirika limebadilika na
mafanikio yanaonekana. Mmedhihirisha kwa vitendo kuwa mashirika ya umma yanaweza
kufanya mambo mazuri. Endeleeni na moyo huo tupate mafanikio zaidi. Kinachotakiwa
ni uongozi mzuri. Mheshimiwa Naibu Waziri;
Ili ujenzi wa nyumba za gharama
nafuu nchini uweze kuwa endelevu ni lazima Serikali iweke mazingira mazuri ya kisera
na kisheria. Inatupasa tuangalie namna ya kupunguza gharama za ujenzi wa nyumba:
kwa upande wa vifaa vya ujenzi kuwa vya gharama nafuu, gharama za viwanja, riba za
mikopo, na kodi mbalimbali. Wizara ishirikiane na Wizara ya Fedha na Benki Kuu na
taasisi za fedha ili kuangalia uwezekano wa kupunguza riba anayotozwa mnunuzi aliyechukua
mkopo benki.
Riba ya asilimia 18 ni kubwa mno. Tafadhali kaeni na taasisi
zinazohusika mjadiliane ili kufanikisha utekelezaji wa sera yetu ya kujenga nyumba
za gharama nafuu. Ni lazima tuendelee na utaratibu huu bila vikwazo ili watu wengi
wanufaike. Maisha bora kwa kila Mtanzania yanahusu pia watu kuwa na nyumba bora za
kuishi.
Vilevile ningependa Wizara yako ihakikishe kuwa Halmashauri zote
nchini zinaharakisha kasi ya upimaji wa viwanja na kuviwekea huduma husika na kuviuza
kwa bei nafuu. Halmashauri zisigeuze bei za viwanja chanzo cha kutafuta mapato na
kumaliza shida zake. Itakuwa vigumu kwa Shirika la Nyumba kujenga nyumba za gharama
nafuu kama Halmashauri zetu zitaendelea kuliuzia ardhi Shirika kwa bei kubwa. Mbona
Halmashauri za Geita, Mvomero, Makete, Kongwa na Mkinga zimeweza kulipatia Shirika
ardhi bila gharama yoyote. Iweje nyingine zishindwe kufanya hivyo? Halmashauri ikiliuzia
Shirika viwanja kwa bei kubwa, gharama za nyumba zinakuwa kubwa na kupoteza dhana
nzima ya unafuu.
Aidha, Wizara inalo jukumu la kuhakikisha kuwa maeneo mapya
yanayopimwa yanakuwa na huduma zote muhimu kama vile umeme, maji, barabara na mawasiliano
ya simu. Huu ni utaratibu wa msingi ambao hautekelezwi ipasavyo. Naomba tuangalia
namna ya kuurejea utaratibu huu kwani utapunguza kero zisizokuwa za lazima.
Pia
naomba Shirika la Nyumba liandae mpango wa ujenzi wa nchi nzima na kisha kuwasilisha
mpango huo Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi mapema iwezekanavyo. Hali
hii itawezesha Wizara na taasisi zinazotoa huduma kuweka mipango yao kulingana na
kazi zilizo mbele yao. Mimi nina imani kuwa Shirika la Nyumba likipewa ushirikiano
mzuri, gharama ya nyumba inazojenga itapungua zaidi. Ndugu wananchi;
Napenda
kuwaahidi kuwa Serikali yenu itaendelea kuboresha sheria na sera mbalimbali ili mazingira
ya kuwekeza kwenye nyumba yaweze kuwa mazuri zaidi. Aidha, tutaendelea kuchukua hatua
zitakazowezesha vyombo vya fedha kupunguza riba ya mikopo wanayotoa. Pia, Serikali
inasubiri mapendekezo ya Kamati niliyoiunda Dodoma kuangalia namna ya kuwezesha ujenzi
wa nyumba za gharama nafuu nchini. Naomba makampuni binafsi nayo yajitokeze kwa wingi
kuunga mkono juhudi zetu. Sisi tupo tayari kushirikiana nao. Mahitaji ni mengi, Shirika
la Nyumba haliwezi kukidhi kiu ya soko la nyumba za gharama nafuu peke yake. Mheshimiwa
Naibu Waziri;
Naomba nimalizie kwa kuwashukuru nyote mlioshiriki katika tukio hili la kihistoria
la uwekaji wa jiwe la msingi katika nyumba za gharama nafuu hapa Kibada. Naona sasa
ndoto yangu ya kuwa na nyumba za gharama nafuu nchini inaanza kutimia. Endeleeni kusimamia
kwa bidii ujenzi wa nyumba hizi. Nyumba huleta amani ya nchi, hivyo tuendelee kutimiza
wajibu wetu kwa kuhakikisha kuwa Watanzania wengi wanamudu kuwa na makazi bora.
Baada
ya kusema hayo sasa napenda kutamka rasmi kuwa niko tayari kuweka jiwe la msingi la
nyumba za gharama nafuu hapa Kibada, ikiwa ni ishara ya kuzindua miradi mingine ya
aina hii inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini. Wananchi watumie
fursa hii vizuri. Nyumba zipo zinaendelea kujengwa nchi nzima.