Kanisa Katoliki Afrika ya Kusini linaandaa Kongamano la Kitaifa ili kujadili kuhusu
Ugonjwa wa UKIMWI, miaka 30 baada ya kugundulika kwake!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Waraka wake Dhamana ya Afrika, Africae
Munus, anahimiza kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini, wenye njaa, wagonjwa hasa
wenye virusi vya Ukimwi na Kifua Kikuu; wakimbizi, wageni na wahamiaji. Kanisa litaendelea
kutoa mchango wake kwa kuzingatia Heri za Mlimani, ambo kimsingi ni muhtasari wa mafundisho
makuu ya Yesu kwa wafuasi wake.
Miaka thelathini imekwisha gota tangu wanasayansi
walipogundua virusi vya ugonjwa wa Ukimwi ambao umeendelea kupukutisha maisha ya watu
kila pembe ya dunia. Katika mapambano haya, Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele
katika kuwahudumia waathirika wa Ugonjwa wa Ukimwi.
Baraza la Maaskofu Katoliki
Afrika ya Kusini, kuanzia tarehe 20 hadi tarehe 22 Januari, 2013 litafanya Kongamano
ili kujadili kuhusu mchango wa Kanisa Katoliki Afrika ya Kusini, miaka thelathini
baada ya kugunduliwa kwa Virusi vya Ukimwi, huko KwaZulu Natal.
Kongamano hili
linatarajiwa kufunguliwa na Monsinyo Roberto Vitillo, mshauri maalum kuhusu ugonjwa
wa Ukimwi kutoka Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa,
Caritas Internationalis, atakayezungumzia kuhusu hali ya ugonjwa wa Ukimwi Kimataifa.
Padre Agbonkhianmeghe Orobator, Kutoka Chuo cha Hekima, Nairobi, Kenya atazungumzia
kuhusu ugonjwa wa Ukimwi kwa Bara la Afrika.
Kardinali Wilfrid Napier atapembua
kuhusu utekelezaji wa mikakati ya mapambano dhidi ya Ukimwi mijini. Askofu Kelvin
Dowling atajielekeza zaidi katika utekelezaji wa mikakati hii vijijini ambako kuna
idadi kubwa ya wagonjwa wa Ukimwi.
Kongamano hili pamoja na mambo mengine litaangalia
kwa undani kuhusu tasaufi, mwelekeo wa kihistoria, maadili katika mapambano dhidi
ya Ukimwi; ushirikiano miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali; mchango wa wanaharakati
wa kike katika mapambano haya; sera za upimaji wa virusi vya Ukimwi; Kanisa na wadau
mbali mbali katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi.