2012-12-12 11:13:39

Kanisa Katoliki Burundi lazindua rasmi Maadhimisho ya Mwaka wa Imani


Baraza la Maaskofu Katoliki Burundi hivi karibuni limezindua rasmi Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kama sehemu ya kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Miaka 20 tangu Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ilipochapishwa kwa mara ya kwanza.

Maadhimisho haya yamefanyika kwenye Parokia ya Muyaga, Jimbo Katoliki la Ruyigi, Burundi. Hii ilikuwa ni parokia ya kwanza kabisa kuwapokea na kuwakaribisha Wamissionari wa kwanza walipofika nchini humo ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu.

Maaskofu Katoliki Burundi wanasema, Mwaka wa Imani kiwe ni kipindi cha kumwilisha Imani katika matendo, sanjari na ujenzi wa maeneo ya kumbu kumbu ya maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kwa sasa na kwa ajili ya kizazi kijacho. Waamini wanapaswa kutambua kwamba, wao ni sehemu ya Familia ya Mungu inayowajibika, changamoto ya kujishikamanisha na kweli za Kiinjili, ili kujenga na kudumisha umoja, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.

Waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee kujitaabisha kuifahamu Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, ili waweze kuitolea ushuhuda Imani wanayoungama katika Fumbo la Utatu Mtakatifu; Imani wanayoadhimisha katika Sakramenti mbali mbali za Kanisa; Imani wanayojitahidi kuiishi kwa kufuata Amri za Mungu dira na kielelezo cha matendo adili pamoja na Imani wanayoisali.







All the contents on this site are copyrighted ©.