2012-12-12 08:52:47

Askofu mkuu Ambrose Madtha kuzikwa India tarehe 14 Desemba 2012


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amepokea kwa majonzi na masikitiko makubwa habari za kifo cha Askofu mkuu Ambrose Madtha aliyekuwa Balozi wa Vatican nchini Pwani ya Pembe, kilichotoea tarehe 8 Desemba 2012 kwa ajali ya gari nje kidogo ya mji wa Abijan.

Baba Mtakatifu ametuma salam za rambi rambi kwa Askofu mkuu Salvatore Pennacchio, Balozi wa Vatican nchini India, ili aweze kumfikishia salam zake za rambi rambi kwa familia, ndugu na jamaa ya Marehemu Askofu mkuu Madtha. Ni kiongozi aliyejitoa kwa ajili ya kudumisha amani na kutafuta mafao ya wengi. Baba Mtakatifu anaungana na wote walioguswa na msiba huu mzito katika kipindi hiki cha maombolezo.

Wakati huo huo, Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican anaungana na wote wanaomboleza msiba huu uliotokea kwa ajali ya gari wakati alipokuwa anatoka kwenye maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili. Anamweka marehemu Askofu mkuu Madtha chini ya maombezi ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, ili aweze kumwombea huruma na hatimaye, kupata tuzo la maisha ya uzima wa milele kutokana na utume wake wa Kipadre.

Marehemu Askofu mkuu Ambrose Madtha anatarajiwa kuzikwa kijijini kwake Belthangady, India, Ijumaa tarehe 14 Desemba, 2012. Mwili wa Marehemu Askofu mkuu Ambrose Madtha unatarajiwa kuwasili nchini India Alhamisi tarehe 13 Desemba 2012.

Rais Alassane Outtara wa Pwani ya Pembe ni kati ya viongozi na waamini waliotuma salam zao za rambi rambi kutokana na msiba huu, kwani Marehemu ni kiongozi aliyejitoa mhanga kwa ajili ya kuendeleza mchakato wa upatanisho, haki na amani nchini Pwani ya Pembe, iliyojikuta katika kinzani na vurugu za kisiasa. Baada ya vurugu zote hizi, alisema, vita imekwisha sasa ni wakati wa kujenga misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa, kila mtu akitekeleza wajibu wake.

Mkakati uwe ni kupania kuondokana na umaskini, ujinga na maradhi maadui makubwa ambao wanaoweza kulitumbukiza taifa katika kinzani na misigano ya kivita. Wananchi wote wa Pwani ya Pembe, wakiwa wameungana na kushikamana; haki msingi za binadamu zikiheshimiwa na kuthaminiwa; hapo kuna kila sababu ya kusonga mbele kwa maendeleo endelevu.







All the contents on this site are copyrighted ©.