2012-12-10 11:04:22

Maboresho ya uhakika na usalama wa chakula Ukanda wa Sahel yanakwenda sanjari na amani na utulivu!


Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO Bwana Josè Graziano da Silva hivi karibuni amesema kwamba, maboresho ya uhakika na usalama wa chakula Ukanda wa Sahel yanaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa amani na utulivu katika Ukanda huu ambao kwa miaka ya hivi karibuni umekuwa ni Uwanja wa Mapambano.

Bwana Da Silva ameyasema hayo wakati akichangia mada kwenye mkutano uliokuwa umeitishwa na Professa Romano Prodi, Mwakilishi maalum wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ukanda wa Sahel, Kaskazini mwa Afrika. Maboresho ya sekta ya kilimo ni mtaji mkubwa unaoweza kusaidia mchakato wa kudumisha amani na utulivu, kwani kuna uhusiano wa karibu sana kati ya baa la njaa na kinzani za kivita; usalama wa chakula na amani Barani Afrika.

Ukanda wa Sahara unakabiliwa kwa kiasi kikubwa na ukosefu wa usalama wa chakula, baa la njaa na umaskini na matokeo yake, rasilimali kidogo iliyopo imekuwa ni chanzo cha kinzani na migogoro katika eneo hili. Usalama wa chakula unakwenda sanjari na usalama pamoja na maendeleo endelevu. Jumuiya ya Kimataifa imekwishachangia kiasi cha Billioni moja za Euro katika kipindi cha mwaka huu na baa la njaa linaendelea kudhibitiwa kwa kiasi kikubwa.

Juhudi hizi hazina budi kwenda sanjari na mikakati ya muda mfupi inayogusa kwa namna ya pekee: usalama wa chakula na lishe; afya, elimu pamoja na usalama. FAO inaendelea kujizatiti kufanya kazi kwa ushirikiano na wadau wengine wa maendeleo na misaada Barani Afrika ili kupata maendeleo ya kweli katika Ukanda wa Sahel.







All the contents on this site are copyrighted ©.