2012-12-07 08:17:36

Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili ni kielelezo makini cha Imani, Matumaini na Mapendo


Mheshimiwa Sr. Palma Porro, Mama Mkuu wa Shirika la Masista wa Bikingira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili la Ivrea anasema, Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili ni wakati wa kufanya tafakari ya kina na kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani.

Karama ya Shirika inawachangamotisha Masista kujitoa bila ya kujibakiza kwa kumuiga Bikira Maria, kielelezo makini cha imani na matumaini kwa Mwenyezi Mungu.

Bikira Maria mkingiwa dhambi ya asili ni kielelezo muhimu cha ubinadamu uliokombolewa kutokana na dhambi na mauti, changamoto ya kujitoa kwa ajili ya kutangaza Injili ya Upendo na Matumaini kwa Mwenyezi Mungu. Ni Mama ambaye alifahamu shida na mahangaiko ya watu wa nyakati zake; akashuhudia kwa mshangao mkubwa, Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo akiteswa na kufa Msalabani, lakini bado akaendelea kubaki na imani thabiti juu ya Mwana wa Mungu, akabahatika kushiriki katika Mpango wa Kazi ya Ukombozi kama wanavyobainisha Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Ni Mama aliyekubali mpango wa Mungu tangu wakati ule alipohabarishwa kuhusu kuzaliwa kwa Masiha hadi pale aliposimama chini ya Msalaba, mwaliko kwa waamii kujitoa bila ya kujibakiza katika huduma inayojionesha kwa namna ya pekee katika hija ya maisha ya imani, utii, upendo na matumaini.

Hata leo hii anasema Mheshimiwa Sr Palma kwamba, inawezekana kabisa mtu kujitoa bila ya kujibakiza katika raha na shida kwa kujichotea nguvu na neema inayopata chimbuko lake katika Sakramenti ya Ubatizo. Ni mwaliko kwa kila mwamini kuchuchumilia utakatifu wa maisha kwa kujitahidi kuwa huru pasi na mawaa ya dhambi.

Ni mwaliko wa kuendelea kufanya hija kutoka katika ubinafsi na usalama na hivyo kujiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu anayeonesha njia ya kupata uhuru kamili, utambulisho wa kibinadamu, furaha ya kweli inayobubujika kutoka katika undani wa mt una amani ya kweli. Imani inamchangamotisha mwamini kujiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu kwa kuonesha uhuru kamili kama alivyofanya Bikira Maria.

Ni kielelezo cha imani na fadhila zilizokomaa na hatimaye, kumwilishwa kwa njia ya huduma ya upendo kwa jirani. Ni Mama aliyeonesha fadhila zote hizi katika uhalisia wa maisha yake. Ni mwanamke aliyekuwa na ukarimu wa ajabu, akaonesha uwepo wake wakati alipohitajika. Alikuwa na upendo mkamilifu, akasamehe na kusahau akiwa na moyo wazi kabisa!

Bikira Maria ni kielelezo cha imani thabiti na majitoleo yanayoonesha njia ya kuweza kukutana na Yesu Kristo na hivyo kuanza kufuata nyayo zake na kuonesha ubinadamu mkamilifu; mwanga wa matumaini thabiti na imani kwa maisha yao kwa sasa kwa siku za usoni.

Mheshimiwa Sr. Palma Porro anaikumbusha Familia ya Waverniani kwamba, uaminifu kwa wito wao, unapata chimbuko lake katika imani na hali ya kujitoa bila ya kujibakiza. Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili ni Mama aliyefanya hija ya imani awasindikize watoto wake katika uhuru wa kweli, ili waweze kuwa ni kielelezo na mfano wa Watoto wa Mungu, Watakatifu na wasio na mawaa katika upendo.








All the contents on this site are copyrighted ©.