2012-12-05 09:01:02

Taasisi za Elimu ya Juu na Vyuo Vikuu ni Jukwaa makini la Uinjilishaji!


Askofu Martin Kivuva wa Jimbo Katoliki Machakosi, Kenya, hivi karibuni alikutana na Wanachuo kutoka Chuo Kikuu cha Daystar waliomtembelea nyumbani kwake, ili kujifunza kuhusiana na masuala mbali mbali ya kichungaji. Askofu Kivuva amekazia umuhimu wa Kanisa kuendeleza shughuli za kichungaji miongoni mwa wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu, kwani hili ni jukwaa muhimu sana la Uinjilishaji ndani ya Kanisa.

Mapadre na Watawa wanaosoma kwenye taasisi na vyuo vikuu, wanapaswa pia kutambua dhamana na wajibu wao wa kuendelea Kuinjilisha kwa njia ya ushuhuda wa maisha na kamwe wasiwakatishe tamaa vijana wengine kutokana na maisha yao ambayo pengine hayamtangazi Kristo kwa umakini mkubwa. Masomo na Uinjilishaji vyuoni ni mambo yanayoweza kwenda pamoja.

Wanafunzi wa taasisi za elimu na vyuo vikuu, sehemu kubwa wanakabiliwa na changamoto ya kumong'onyoka kwa misingi bora ya maadili na utu wema; kupenda mno malimwengu; matumizi haramu ya dawa za kulevya, ukahaba pamoja na matumizi mabaya ya rasilimali fedha wanayopewa wakati wakiwa masomoni. Hizi ni dalili ambazo zinaonesha haja kwa Mama Kanisa kujipanga vyema zaidi, ili kuwasaidia wanavyuo kutambua na kuthamini uwepo wao vyuoni kama mahali pa kujipatia elimu, ujuzi na maarifa pamoja na kuimaarisha imani yao, kwa njia ya ushuhuda amini wa maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.