2012-12-05 13:43:50

Iweni mashahidi wa Kristo kwa njia ya: Imani. Mapendo na Matumaini


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa katekesi yake, Jumatano tarehe 5 Desemba 2012 katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ametafakari kuhusu Kipindi cha Majilio, kinachowakirimia waamini fursa ya kufanya tafakari ya kina kuhusu ukuu wa Mungu katika Mpango wa Ukombozi. Utenzi unaofungua Waraka wa Mtakatifu Paulo kwa Waefeso, unamshukuru Mwenyezi Mungu kwa huruma na mapendo yake makuu aliyewachagua katika Kristo kabla ya kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu ili kuwafanya kuwa ni watoto wake.

Baba Mtakatifu anasema, Mpango wa Mungu ni kuvijumuisha vitu vyote katika Kristo. Mwenyezi Mungu ameufunua Mpango wake kwa njia ya Ufunuo unaopata hitimisho lake katika Fumbo la Umwilisho wa Mwana wa Mungu na kwa njia ya ujio wa Roho Mtakatifu. Kujifunua kwa Mwenyezi Mungu kwa njia ya Yesu Kristo ni kuna endana na matumaini pamoja na matamanio ya binadamu; mwaliko kwa waamini kuweza kuitikia kwa kuonesha utii wa Imani kwa Mwenyezi Mungu.

Kitendo cha mwamini kuinua akili na utashi wake kwenye ufunuo wa Kimungu; ni mwaliko wa kiimani kutubu na kuanza kuona ukweli wa maisha na ulimwengu unaowazunguka kwa mtazamo mpya. Kipindi hiki cha Majilio, ni mwaliko wa kufanya tafakari ya kina kuhusu uzuri wa Upendo wa Mungu katika kazi ya Ukombozi sanjari na kujitahidi kuwa ni alama hai ya uwepo wake ulimwenguni.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwa njia ya upendo, imani na matumaini wanaweza kuwa ni mashahidi wa uwepo wa Mungu duniani.

Amewashukuru kwa namna ya pekee, mahujaji waliofika mjini Roma, kama sehemu ya maadhimisho ya kutangazwa kwa Mtumishi wa Mungu Sista Maria Crescenzia Perez kuwa Mwenyeheri, changamoto na mwaliko kwa kufuata nyayo zake kwa uaminifu na furaha, huku wakijitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza Injili. Amelishukuru Shirikisho la Waoka Mikate Italia kwa zawadi ya mikate waliyompatia kwa ajili ya huduma ya upendo wa Papa.







All the contents on this site are copyrighted ©.