2012-12-03 08:07:37

Majaalim wabainisha changamoto wanazokabiliana nazo katika sekta ya elimu ya juu


Professa Paolo Paris, Mkuu wa Chuo Kikuu cha “Foro Italico”, akizungumza kwa niaba ya walezi wenzake kutoka katika taasisi na vyuo vikuu vilivyoko mjini Roma, wakati wa Masifu ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumamosi tarehe Mosi Desemba, 2012 anasema kwamba, kwa sasa wanakabiliana na kinzani zinazohatarisha urithi, mfumo, maudhui pamoja na malengo ya majiundo kwenye vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu.

Kuna wakati vyuo vikuu lilikuwa ni jukwaa la majiundo makini, mahali pa upembuzi yakinifu pamoja na kurithisha ujuzi na maarifa. Ilikuwa ni fursa ya kukua na kukomaa kitamaduni na kimaadili; lakini leo hii, misingi hii iko hatarini kwani inapimwa na mizani ya maendeleo, fursa za ajira, usawa, mshikamano, uhusiano wa dhamiri ya mtu na sheria maadili pamoja na mambo kadhaa yanayowazunguka wakati mwingine yakiwa na mwelekeo hasi zaidi.

Vyuo vikuu vinachangamotishwa kutambua na kuthamini uwepo wa Mwenyezi Mungu na kwamba, mwanadamu ana kiu ya kutaka kuonana naye. Kongamano la Majaalim Kimataifa, litakuwa na wajibu wa kubainisha umuhimu wa tamaduni mbele ya Mweyezi Mungu. Huu utakuwa ni mchango makini wakati wa maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Professa Paris anasema, ulimwengu mamboleo umegubikwa mno na ubinafsi, madhara yake wakati mwingine yanajionesha hata katika Kanisa, ambalo vijana wanaliona kuwa ni kielelezo cha matumaini. Hili ni Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya linaloalikwa kuunda watu wenye utu mpya unaowawajibisha kijamii, kwa kutoa majibu makini yanayopata chimbuko lake katika maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili mintarafu utendaji wa shughuli za kijamii.

Huu ni mwaliko wa kuendeleza majadiliano, kwa kutafuta zaidi, kile kinachowaunganisha ili kuvuka vikwazo na kinzani zisizo na tija, kwa ajili ya maisha ya mwanadamu. Walezi hao wametumia fursa hii kumtakia matashi mema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika kipindi hiki cha Majilio na hatimaye, wakati wa maadhimisho ya Sherehe za Noeli kwa Mwaka 2012.








All the contents on this site are copyrighted ©.