2012-12-01 08:49:17

UNICEF yasema, maambukizi mapya ya Virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa Mtoto yamepungua, lakini lengo bado halijafikiwa!


Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF linabainisha kwamba, maambukizi ya virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa mtoto yamepungua, lakini lengo kuu la UNICEF ni kuhakikisha kuwa Jumuiya ya Kimataifa inakuwa na kizazi kisichokuwa na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi. Lengo hili linaweza kutimia ikiwa kama wanawake wajawazito na watoto walioathirika kwa Virusi vya Ukimwi watapata matibabu muafaka.

Takwimu zinaonesha kuwa, maambukizi ya Virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa mtoto wakati wa kujifungua yamepungua kwa asilimia ishirini na nne katika nchi ishirini na mbili na nyingi kati ya hizi ni zile ambazo ziko Kusini mwa Jangwa la Sahara. Jumuiya ya Kimataifa anasema Bwana Anthony Lake, haina budi kuhakikisha kwamba, inatoa dawa kwa watu wazima, ili kusaidia kufanikisha mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi duniani. Watoto wapimwe na kupewa huduma stahiki kadiri ya mikakati ya Umoja wa Mataifa.

Huduma ya afya kwa wanawake wajawazito wenye Virusi vya Ukimwi, itawawezesha wanawake hawa kuishi kwa muda mrefu zaidi pamoja na kutoa hifadhi kwa watoto wao, ili wasiambukizwe na Virusi vya Ukimwi. Lengo liwe ni kuhakikisha kuwa, hakuna tena maambukizi mapya ya Virusi vya Ukimwi, ifikapo mwaka 2015.







All the contents on this site are copyrighted ©.