Kipindi cha Majilio ni mwaliko wa kufanya toba na wongofu wa ndani
Kardinali Angelo Scola, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milano, Italia, katika kipindi
cha Majilio anawaalika waamini kujitaabisha kuutafuta ili hatimaye, kuuona wokovu
unaoletwa na Masiha, kwani kila mtu atauona. Ni ufalme unaojikita katika misingi ya
haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati miongoni mwa Watu wa Mataifa.
Hii
ni kutokana na ukweli kwamba, wokovu ni kwa watu wote, kwani hii ni zawadi kutoka
kwa Mwenyezi Mungu inayopata utimilifu wake kwa njia ya Yesu Kristo Mkombozi wa Dunia.
Kwa njia ya Kanisa, wote wanapata fursa ya kufanyika Watoto wa Mungu na hivyo wanatumwa
kwenda duniani kote kutangaza Habari Njema ya Wokovu, kwani Ukristo ni dini ya watu
kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu, kama ambavyo aliwahi kusema, Baba Mtakatifu Paulo
wa sita.
Kiini cha Habari Njema ya Wokovu ni Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka
kutoka katika wafu, atarudi tena kuwahukumu wazima na wafu na wala ufalme wake hautakuwa
na mwisho. Ili kufanikiwa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu, kuna
haja ya kufanya toba na wongofu wa ndani. Hii ndiyo njia iliyooneshwa na Yohane Mbatizaji
wakati alipokuwa anahubiri kuhusu Ubatizo wa Toba kwa maondoleo ya dhambi, jambo ambalo
linakamilika hatua kwa hatua. Toba na mwongofu wa ndani ni mambo yanayomwezesha mwamini
kubadili mtindo na mfumo wa maisha yake, akijitahidi kukumbatia utakatifu wa maisha.
Yohane
Mbatizaji anatangaza ujio wa Masiha atakayebatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa njia ya
Maji ya Ubatizo, watu wanafanyika kuwa ni Watoto wa Mungu na hivyo kustahilishwa kushiriki
katika matunda ya ahadi zilizotolewa wakati wa Agano kati ya Mungu na Waisraeli.
Kardinali
Angelo Scola anasema, Kipindi hiki cha Majilio kwa namna ya pekee kabisa, kinaendeleza
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliozinduliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, sanjari na Uinjilishaji Mpya unaopaswa kutekelezwa na Mama Kanisa
katika maisha na utume wake.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati
wa Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu kufunga Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu
juu ya Uinjilishaji Mpya alikumbusha kwamba, kuna umati mkubwa wa watu wanaohitaji
Kuinjilishwa Upya; Yaani wana kiu na njaa ya kutaka kukutana na Yesu Kristo, Mwana
wa Mungu, ili aweze kufungua macho yao pamoja na kuwafundisha njia wanayopaswa kuifuata
katika hija ya maisha yao baada ya kumezwa na malimwengu, kiasi kwamba, ule moto wa
Mungu uliokuwa umewashwa ndani mwao, unaonekana kuzima.
Watu wanahitaji kupata
joto la Habari Njema ya Wokovu, kwa ajili yao wenyewe pamoja na Familia zao. Moto
wa Imani uliowashwa miaka kadhaa iliyopita, unaendelea kufifia, hatari kwa waamini
wanaoishi katika ulimwengu mamboleo! Kumbe, Uinjilishaji Mpya ni dhamana ya Wakristo
wote.
Kardinali Angelo Scola anabainisha kwamba, Imani ni jibu makini kwa
mahangaiko ya watu wa nyakati hizi. Kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa
kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa kwa njia ya ushuhuda wa maisha
kwa Kristo na Kanisa lake, ili kuhakikisha kwamba, kila mtu anauona wokovu, ili hatimaye,
aweze kukombolewa kwa njia ya Yesu Kristo, anayewaonjesha upendo na huruma ya Baba
yake wa mbinguni.
Kuna maovu yanayoendelea kutendeka hapa duniani. Ikumbukwe
kwamba, haki na huruma ni chanda na pete. Msamaha wa Mungu ni jinsi ambavyo Mwenyezi
Mungu anatenda ili kumwokoa mwanadamu kutokana na mapungufu yake yaliyopita, kwa kutambua
kwamba, anapaswa kushiriki kikamilifu katika kazi ya ukombozi, Mungu alimuumba mwanadamu
pasi na ridhaa yake, lakini hawezi kumkomboa bila ushiriki wake.
Waamini wakati
huu wa Kipindi cha Majilio, watambue mapungufu na dhambi zao, wakimbilie huruma na
upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho, kama njia ya kujiandaa kumpokea
Masiha na Mkombozi anayekuja Ulimwenguni.