2012-11-30 08:56:45

Siku ya mshikamano wa Kimataifa na Wapalestina


Miaka sitini na tano imekwisha yoyoma tangu Umoja wa Mataifa ulipopitisha Azimio namba 181 lililogawanya Israeli na Palestina, anasema Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon katika ujumbe wake kwa ajili ya maadhimisho ya Siku ya Mshikamano wa Kimataifa na Palestina, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 29 Novemba.

Anasema, Palestina bado inaendelea kukabiliana na hali ngumu ya maisha pamoja na vikwazo mbali mbali, hii yote ni kutokana na Jumuiya ya Kimataifa kushindwa kutoa suluhu ya kudumu kutokana na kinzani hizi.

NI matumaini ya Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa kwamba, Mataifa haya mawili yatajitahidi kukoleza utashi wa kisiasa; ari na moyo wa ujasiri, kila upande ukiwajibika kupania kujenga na kudumisha amani ya kudumu kati ya nchi hizi mbili ambazo zimekuwa zikisigana mara kwa mara wakiwa na matumaini kwa vijana wa kizazi kipya. Majadiliano ya kina ndiyo dawa pekee ya amani, utulivu na usalama huko Mashariki ya Kati.

Nchi hizi mbili zijitahidi kudhibiti biashara haramu ya silaha; kubomoa ukuta unaowatenganisha pamoja na kuharakisha mchakato wa upatanisho miongoni mwa Wapalestina. Serikali ya Palestina inawajibika anasema Katibu mkuu kujenga miundo mbinu itakayorahisisha utekelezaji wa shughuli zake, daima ikijitahidi kuheshimu Sheria za Kimataifa. Haki, Amani na Utulivu ni nguzo muhimu kwa ajili ya ustawi wa Wananchi wa Palestina.







All the contents on this site are copyrighted ©.