2012-11-29 14:11:47

Kenya: Askofu ahimiza uinjilishaji kupitia vyombo vya mawasiliano.


Askofu Emmanuel Barbara (OFM), wa Jimbo Katoliki la Malindi Kenya , amehimiza waamini Katoliki, kuvitumia vyombo vya habari kueneza Ujumbe wa Habari njema ya Injili.

Himizo hili alilitoa wakati wa kuzindua warsha ya Kijimbo, iliyofanyika katika Kituo cha Kichungaji cha Malindi, Ijumaa iliyopita Novemba 23 , na kuhudhuriwa na wanahabari kutoka Jimbo la Malindi na Jimbo Kuu la Mombasa.

Jimbo kuu la Mombasa hujumuiya majimbo Katoliki ya Malindi, Mombasa na Garissa, Katika warsha hii, wanahabari kutoka jimbo la Garissa hawakuhudhuria kutokana na ukosefu wa usalama katika eneo lao lililotajwa kuwa katika hali ya hatari na hivyo watu wamekatazwa kutembea ovyo.

Wakati wa Warsha Askofu Barbara, alivitaja vyombo vya mawasiliano kuwa na uwezo mkubwa wa kuwaunganisha watu, kama inavyoonekana sasa kwamba, vimewezesha dunia kuwa kijiji kidogo na kujenga umoja na mshikamano zaidi kati ya watu. Kwa manufaa hayo, pia vinaweza kutumika katika kueneza haraka Neno la Mungu.

Alisema, hii ni njia inayofaa kueneza haraka ujumbe wa Injili kwa watu wote. Na hasa Redio, inao uwezo wa kupenyeza ujumbe kwa familia nyingi bila lazima ya kuonana ana kwa ana na familia, hasa zilizoko katika maeneo ya ndani vijijini na pia maeneo hatarishi. Na hivyo njia hii ya redio inarahisisha kazi ya kuinjilisha.

Askofu Barbara, alieleza na kutaja jinsi Baba Mtakatifu Benedikto XV1, alivyojiunga na tovuti ya Facebook na hivyo kuliinua jukwaa la wanahabari wa kanisa katika uwanja mpya wa mawasiliano.

Na aliitaja changamoto inayowakabiliwa wanamawasiliano wa Kanisa , ni kufika katika vyombo vya habari, na kuanzisha mijadala juu ya amani na ukweli.







All the contents on this site are copyrighted ©.