2012-11-28 11:47:02

Umaskini unavyowatikisa watu Barani Ulaya!


Kwa nini umaskini?
Hili ni swali msingi ambalo Shirikisho la Watangazaji Ulaya, “European Broadcasting” EBU linawaalika watu kulitafakari kupitia vyombo mbali mbali vya habari, hapo tarehe 29 Novemba 2012. Umaskini ni jambo la zamani, lakini linafumbata mambo mapya kwa sasa. Kuna wakati ambapo watu wengi waliufumbia macho umaskini sehemu mbali mbali za dunia; lakini leo hii, wananchi wanaoishi katika Nchi Tajiri zaidi duniani, wanachangamotishwa na Serikali zao pamoja na Mashirika ya Fedha Kimataifa kujifunga mikanda ili kukabiliana na hali ngumu ya maisha.

Huu ndio ule wimbo uliombwa kwenye miaka 80/90 kwa nchi nyingi za Kiafrika, walipoambiwa kujifunga mkanda, kiasi kwamba, baadhi ya nchi kama vile Msumbiji wakasema, kwa hakika, watu wanapoteza maisha yao kutokana na masharti magumu ya kiuchumi yanayotolewa na Taasisi za Fedha Kimataifa.

Katika kipindi cha Mwaka 1994, uwezo wa kununua bidhaa na huduma kwa wananchi wanaozungumza lugha ya Kifaransa, ukashuka kwa asilimia 50%; matokeo yake, mfumuko wa bei ya bidhaa na huduma ikapaa juu maradufu! Wakasema, ni matokeo na athari za Ukoloni. Wananchi hawa ambao wamekuwa sugu kutokana na umaskini na hali ngumu ya maisha kutoka katika Nchi Maskini duniani, kilio chao hakikusikilizwa, ikawa ni sawa na machozi ya Samaki kuishia majini.

Takwimu zinabainisha kwamba, kati ya nchi 44 Maskini zaidi duniani, kati yake nchi 33 zinapatikana Barani Afrika. Umaskini huu wanasema kwamba, ni matokeo ya: utawala mbaya, udikteka, vita, kinzani na migogoro ya kikabila; mgawanyo na matumizi tenge ya rasilimali ya nchi; rushwa na ufisadi; wasomi wengi kukimbia nchi zao kwa kutafuta malisho ya kijani kibichi ughaibuni; uhusiano tenge wa shughuli na mikakati ya kiuchumi na nchi za Bara la Afrika; ukwapuaji wa malighafi toka Barani Afrika; ukoloni na athari zake. Hali hii pia inajitokeza katika Nchi za Amerika ya Kusini na Asia, ambazo zilipachikwa jina na kuitwa Nchi Zilizoko Dunia ya Tatu, “LDC”.

Wasomi wengi waliangalia mwenendo huu wa uchumi kwa macho ya makengeza, kwani kuwa watu waliokuwa wanaishi katikati ya dunia na wengine walisukumizwa pembezoni kabisa mwa dunia; lakini bado zikaendelea kutegemeana katika uwiano tenge, kiasi cha kuanza kuibua hisia ya kutaka uwepo Mfumo Mpya wa Uchumi Kimataifa, “NIEO”, bila shaka wachumi wengi watakumbuka mwenendo huu, lakini wazo hili halikuweza kufanyiwa kazi, ili kuleta uwiano bora na tengamanifu katika masuala ya kiuchumi. Ndiyo maana EBU linauliza tena leo hii “Kwa nini Umaskini?”

Hapa tunazungumzia umaskini wa hali na kipato, unaoendelea kugusa mamillioni ya watu kutokana na kukoswa fursa za ajira katika Nchi ambazo, hadi siku za hivi karibuni, zilijulikana kama Nchi Tajiri Duniani; mahali ambapo watu walikuwa kuku kwa mrija! Wananchi kutoka Afrika, Asia na Amerika ya Kusini, wakaendelea kuambulia pakavu! Umaskini wa kiuchumi ni chanzo cha mtikisiko huu, ambao pia umechangiwa na mambo mengine msingi katika maisha ya mwanadamu.

Kwa miaka mingi Kanisa lilihimiza maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili; kitamaduni na kijamii. Mtu na utu wake hana budi kuwa n ikiini cha mikakati ya maendeleo, vinginevyo ni kupoteza dira na hatimaye, kukosa mwelekeo. Kanisa liliona na kutambua madhara na hatari katika maisha ya kijamii, kwenye uchumi uliokuwa unakumbatia mfumo wa Ubepari uliokuwa unajikita katika faida kubwa, pasi ya kujali misingi ya maadili na utu wema! Matokeo yake ni kilio kinachoendelea kusikika kutoka sehemu mbali mbali za dunia baada ya kuguswa na makali ya kuchechemea kwa uchumi wa kimataifa!

Haya ni matokeo ambayo baadhi ya wanazuoni kutoka Afrika kama vile Engelbert Mveng wanauita ”Umaskini wa Kiutu”, yaani ni umaskini ambao umemtikisa mwanadamu katika undani wa maisha yake; katika jinsi ya kufikiri na kutenda; katika kujiwekea mikakati yake kwa siku za usoni. Wale ambao walidhani kwamba wameupatia umaskini kisogo, leo hii wanaguswa na kutikiswa vibaya sana, kwa sababu binadamu wote ni sawa! Waswahili wanasema, eti kutesa kwa zamu! Kama anavyokiri pia C. Hamidou Kane katika kitabu chake kijulikanacho kama ”L’aventura Ambigua”

Kuna haja ya kuweka uwiano bora zaidi kati ya nchi zilizoendelea na maskini zaidi duniani, kwa kuhakikisha kwamba, kuna kuwepo na ugavi bora wa rasilimali ya dunia unaozingatia msingi wa haki na mshikamano unaoongozwa na kanuni. Watu wanapaswa kujifunza kuwa na kiasi na kwamba, hata katika umaskini, bado watu wanaweza kuthamini utu na heshima ya mwanadamu.

Hii ni changamoto iliyokuwa imetolewa kunako mwaka 1978 na Albert Tèvoèdjirè katika kitabu chake ”La povertà, Ricchezza dei Popoli” Huu ni umaskini jeuri, unaomwezesha mtu kuthamini utu na heshima yake na kwamba, mali si kipimo cha utu; mwaliko wa kutumia utajiri nam ali ya dunia kama kielelezo cha mshikamano wa upendo na ”akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi”, wanaoendelea kuongezeka siku hadi siku! Kila mtu atambuliwe, aheshimiwe na kuthaminiwa.

Huu ndio muhtari wa Mafundisho Jamii ya Kanisa unaojikita katika Kweli za Kiinjili na kwamba dunia itapita, lakini Neno la Mungu litabaki Imara. Mtikisiko wa uchumi kimataifa, uikumbushe Jumuiya ya Kimataifa kwamba, wote wanasafiri katika mtumbwi mmoja kama binadamu, kwa kushikamana kwa pamoja, wanaweza kuokoka, lakini kila mtu akijitafuta mwenyewe, matokeo yake ni kuangamia. Watu waufahamu umaskini na changamoto zake, pengine ni huduma makini ambayo EBU imetoa kwa Jumuiya ya Kimataifa, kwa kuuliza swali msingi ”kwanini umaskini”?

Tahariri hii imeandaliwa na Dr. Maria Dulce Araujò Evora kutoka Idhaa ya Kireno ya Radio Vatican na kutafsiriwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.